Wizara ya Maliasili na Utalii imesema kuwa imepokea maoni yatakayosaidia kuboresha mapendekezo ya marekebisho ya Kanuni za Uwindaji wa Wenyeji nchini kupitia mifumo ya Kisheria iliyopo.

Akifungua kikao cha Wawindaji Wenyeji, Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe Balozi Dkt. Pindi Chana (Mb) amesema kuwa Serikali kwa kutambua umuhimu wa wenyeji kunufaika na rasilimali za wanyamapori kama ilivyoainishwa katika Sera ya Wanyamapori ya mwaka 2007, iliamua kuanzisha utaratibu wa uwindaji wa wenyeji ili kuwawezesha wenyeji na wageni wakazi kupata kitoweo cha nyamapori kwa utaratibu rahisi na kwa bei nafuu bila kuathiri dhana nzima ya uhifadhi endelevu.

“Serikali ilitenga maeneo ya wazi yatumike kwa ajili ya shughuli za uwindaji wa wenyeji kupitia utaratibu maalum ambao uliwekwa katika Kanuni za mwaka 2010” Amesema Mhe. Balozi Dkt Chana

Aidha, Waziri Balozi Dkt. Chana amewataka wadau hao kutumia fursa hiyo kutoa maoni ya kujenga na ambayo yatazingatia mahitaji na malengo ya uwindaji wa wenyeji kwa kuzingatia mustakabali mzima wa uhifadhi kwa manufaa na kizazi cha sasa na kijacho

Kikao kazi hicho kilichofunguliwa Jijini Arusha, kimejumuisha wataalam kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, TAWA, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Wadau wa uwindaji wa wenyeji.