WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka wakuu wa mikoa iliyopo mipakani watekeleze maelekezo ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ya kufanya ufuatiliaji wa watu waliounda vikundi visivyo rasmi vinavyosababisha migogoro katika sekta ya usafirishaji.

Amesema kuwa Serikali haitomvumilia mtu yeyote anayejihusisha na vitendo hivyo vilivyo tofauti na sheria na taratibu za nchi. “Ukifanya vitendo viovu utajiingiza kwenye migogoro, kuwa makini usijeingia kwenye mgogoro kwa kutumwa tu, tunazo sheria za nchi.”

Amesema hayo  Jumatano Julai 27, 2022 alipofanya ziara ya kawaida ya Kukagua mwenendo na shughuli za usafirishaji katika Halmashauri ya Mji wa Tunduma Mkoani Songwe.

Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa iwapo kuna changamoto yoyote katika sekta ya usafiri inayowahusisha madereva na waajiri wao wasisite kuziwasilisha Serikalini. “Kama zipo shida njooni sisi tutawapokea na kuwasikiliza ili kutatua shida zenu, malori yanayotoka na kuingia nchini yaachwe, tusijihusishe na migogoro ambayo inatatulika.”

Aidha, Waziri Mkuu amewapongeza madereva kwa kuamua kuisikiliza Serikali na kurejea kwenye shughuli za usafirishaji kama awali.

“Taifa linakua kiuchumi katika sekta nyingi ikiwemo sekta ya usafirishaji, kuzuia wengine kufanya kazi ya usafirishaji ni uhujumu uchumi, magari haya yanatuletea fedha, kwani yanahudumiwa na wananchi wengi ambao kwa kufanya hivyo wanajipatia fedha na kuendesha maisha yao”

Ameongeza kuwa sekta binafsi inashamiri zaidi nchini na kuwa ni sehemu ya ukuaji wa uchumi. “Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan inatambua na itaendelea kuweka mazingira mazuri ili Watanzania waendelee kunufaika, lengo ni kupanua uchumi kutoka kwa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla”

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, David Silinde amesema kuwa katika kipindi cha mwaka mmoja wa Rais Samia, Serikali imejenga shule katika kata 466 mpaka sasa na ujenzi wa vituo vya afya 234 nchi nzima”