Na Tiganya Vincent-Mahakama ya Tanzania

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Wilbert Chuma amewataka watumishi wa Mahakama wapya kufanyakazi kwa uadilifu na maadili mema kwa kuepuka kufanya vitendo ambavyo vinaweza kuwavunjia heshima kwa  jamii wanayoitumikia.

Amesema kuwa kwa upande wa Mahakimu ni vema wakazingatia maadili ambayo kimsingi yanawataka kupunguza marafiki na kujitoa kwenye mambo mengi ya kijamii kama vile makundi ya Whatsapp, washirika wa kibiashara na starehe ambazo zinaweza kutia doa taswira ya Mahakama.

Kauli hiyo imetolewa Mjini Lushoto na Mhe. Chuma wakati akifungua mafunzo elekezi kwa Mahakimu wakazi Wasaidizi wa Kumbukumbu walioajiriwa hivi karibuni

Amewataka waajiriwa wapya kujenga tabia ya kujifunza na kujua utamaduni wa Mahakama (judicial culture) na kuuishi huku wakizingatia mipaka ya kazi zao na kila mmoja akiheshimu na kulinda mipaka ya wengine.

Mhe. Chuma amesisitiza kuwa nidhamu ya kazi inaendana pia na kuheshimu watumishi wenzao na kutumia muda wa mwajiri ili kuifanya Mahakama iendelea kukubalika kwa jamii inayowatumika na kufikia malengo na dira yake.

Msajili Mkuu huyo wa Mahakama ya Tanzania ameongeza kuwa Mahakimu lazima watambue kuwa wao pia ni Viongozi wa umma ambao wanapaswa kuhakikisha kuwa wanapokuwa mahakamani hawavunjii heshima , kuwadhalilisha watu bila kujali ni wakili, shahidi, mshtakiwa, mtumishi wa Mahakama na hata hakimu mwenzio.

Mhe. Chuma amesisitiza majukumu yao kwa mujibu wa sheria za nchi  kwa ngazi mbalimbali katika kufikia azma ya kutenda na kutoa haki kwa mujibu wa sheria na wasiwe chanzo cha malalamiko au kusababisha uvunjifu wa amani kutokana na utendaji kazi wa baadhi yao ambao unakiuka misingi ya utu na katiba.

Aidha Mhe. Chuma amewataka Waajiri wapya kufanya kazi kwa  ushirikiano na watumishi watakaowakuta katika maeneo ya kazi ili kuhakikisha Mahakama inandelea kutoa huduma nzuri ya utoaji haki kwa wananchi.

Amesema ushirikiano na wenzao watakaowakuta  kwenye vituo vyetu vya kazi utasaidia kufanikisha jitihada zinazoendelea kuhusu maboresho ya Mahakama ya Tanzania na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo na kusogezaji wa utoaji haki karibu na wananchi.

Watumishi hao wapya watapata fursa ya kujifunza mada zinazogusa maisha yao binafsi mfano kujilinda na msongo wa mawazo na kuwa na nidhamu binafsi ya matumizi ya fedha pamoja na mambo mengine.

Vilevile watafundishwa mada mahususi zinazohusu taaluma zao ambazo ni pamoja na usikilizaji wa mashauri ya madai ya kawaida, ndoa, jinai, talaka, mirathi, uandishi wa hukumu na utoaji wa adhabu.