Watu watatu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi wameuawa katika eneo la Goba wilayani Kinondoni mkoani Dar es Salaam, wakati wa majibizano ya risasi na polisi.

Kamanda wa polisi kanda maalum ya Dar es Salaam Muliro Jumanne amewaambia waandishi wa habari kuwa, watu hao walikuwa katika harakati za kuiba kwenye duka linalojulikana kama Sky Matty.

Amesema polisi walifanikiwa kuwadhibiti watuhumiwa hao wa ujambazi kutokana na ushirikiano walioupata kutoka kwa wananchi.

Kwa mujibu wa kamanda Muliro, askari mmoja amejeruhiwa katika tukio hilo na kwa sasa anaendelea kupatiwa matibabu.