Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Tulia Ackson amesema kwa sasa Tanzania ina maelewano mazuri na jirani zake na si vinginevyo.

Spika Tulia amelazimika kutoa kauli hiyo bungeni jijini Dodoma baada ya mbunge wa viti maalum Agnes Marwa kudai bungeni kuwa baadhi ya nchi jirani na Tanzania zimeanza chokochoko.

Ametoa madau hayo wakati akichangia mjadaka wa bajeti kuu wa serikali kwa mwaka wa fedha wa 2022/2023 katika sekta ya utalii.

“Huu ni mhimili wa bunge na hizi taarifa zimekuja kwa njia za mitandao, bunge haliwezi kujibu chokochoko za mitandao kwa kutumia bunge, wabunge tujikite katika hoja zetu za maendeleo ya nchi yetu, mpaka sasa bunge taarifa iliyonayo ni ile aliyotoa Waziri Mkuu hapa bungeni, hiyo ndio taarifa ya serikali kuhusu Ngorongoro na Loliondo.” amesema Spika Tulia

Pia Spika amesema kwa hizo chokochoko anaona ni vema wenye nia ya kujibu waende kwenye taarifa husika zilipotoka (mitandao) ili wakajibu huko na sio kutumia mhimili wa bunge.