OFISI ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI) imetangaza majina 16,676 ya watumishi wapya waliopangiwa vituo vya kazi katika Sekta ya Elimu na Afya nchini.

Orodha hiyo inatokana na waombaji wenye sifa waliokidhi vigezo baada ya Aprili, 2022 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan kutoa kibali cha ajira kwa kada za Ualimu na Afya, kwa ajili ya kuajiri walimu 9,800 wa shule za msingi na sekondari na wataalam wa afya 7,612.

  
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mheshimiwa Innocent Bashungwa amesema, baada ya kupata kibali cha ajira, Ofisi ya Rais-TAMISEMI ilitoa tangazo kwa wahitimu mbalimbali wa Ualimu na Kada za Afya, kuwasilisha maombi ya kazi, kupitia mfumo wa kielektroniki wa kupokea na kuchakata maombi ya ajira, kuanzia Aprili 20 hadi Mei 8,2022.

Mheshimiwa Bashungwa akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma Juni 26, 2022 amesema, jumla ya maombi 165,948 yakiwemo ya wanawake 70,780 na wanaume 95,168 yaliyopokelewa kwenye mfumo, ambapo maombi ya kada za afya ni 42,558, na kada ya Ualimu ni 123,390.

Amesema, kwa upande wa kada za ualimu,waombaji wenye sifa waliokidhi vigezo na kupangiwa vituo vya kazi ni 9,800 ambapo jumla ya walimu 5,000 wamepangwa shule za msingi na walimu 4,800 Shule za sekondari, wakiwemo walimu wenye ulemavu wa shule za msingi na sekondari 261.

==>BOFYA HAPA KUTAZAMA MAJINA YA WALIOCHAGULIWA
 
 Waziri Bashungwa amesema, kwa upande wa kada za Afya,waombaji wenye sifa waliokidhi vigezo na kupangiwa vituo vya kazi ni 6,876 wanawake ni 3,217 sawa na asilimia 46.8 na wanaume ni 3,659 sawa na asilimia 53.2 wakiwemo wenye ulemavu 42 sawa na asilimia 0.61.

Mheshimiwa Waziri Bashungwa amesema, ili kufanikisha mchakato wa ajira, Ofisi ya Rais-TAMISEMI iliunda Timu Maalum, ya kufanya Uchambuzi wa Maombi ya Ajira, iliyohusisha taasisi mbalimbali.

==>BOFYA HAPA KUTAZAMA MAJINA YA WALIOCHAGULIWA
 
 Taasisi hizo amesema, ni pamoja na Ofisi ya Rais Ikulu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU), Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA), Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Ufundi Stadi (NACTVET), Sekretarieti ya Ajira, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), na Mabaraza ya Kitaalamu katika Sekta ya Afya.

Waziri Bashungwa amesema, kutokana na idadi ya waombaji kuwa kubwa, Timu ya Uchambuzi wa Maombi ya Ajira ilipewa vigezo vilivyoandaliwa kama mwongozo wa kutoa ajira kwa waombaji, kwa lengo la kuhakikisha uwepo wa haki na uwazi katika zoezi hili.

Amesema, katika kuhakikisha usawa wa kijinsia unafikiwa, katika vigezo vilivyotumika kupata waajiriwa wapya kwa mwaka 2022, kila kigezo kilizingatia uwiano wa  kijinsia.