Balozi wa Tanzania Nchini Malawi Mhe. Humphrey H. Polepole amekutana na kufanya mazungumzo na Mhe. Nancy Tembo (Mb) Waziri wa Mambo ya Nje wa Malawi.

Balozi Polepole na Mhe. Tembo pamoja na mambo mengine, wamezungumzia dhamira njema ya Tanzania na Malawi katika kuimarisha mahusiano yake ya kidiplomasia, kiuchumi, kibiashara na ujirani mwema.

Mazungumzo yamejikita pia katika vikao vya pamoja vya kukuza na kuendeleza mahusiano vinatarajiwa kufanyika baadaye mwaka huu na kuendelea kufuatilia utekelezaji wa mikataba (MoUs) ya Kimaendeleo ambayo imekwisha kubaliwa baina ya Tanzania na Malawi.

Mhe. Polepole amemhakikishia kwamba maelekezo ya Serikali ya Tanzania ni kuendeleza na kukuza mahusiano imara na madhubuti yaliyopo na ambayo yamekuwa yakiwanufaisha Kiuchumi na Kimaendeleo wananchi wa pande zote mbili, Tanzania na Malawi.

Wakati uo huo Mhe. Polepole amepokea ujumbe wa Waalimu 21 wa Skuli za Awali, Msingi na Sekondari kutoka Zanzibar ambao wako katika ziara ya mafunzo kwa vitendo Nchini Malawi.

Ubalozi umejipanga pamoja na mambo mengine katika Uhusiano wa Tanzania na Malawi kukisogeza Kiswahili nchini hapa ili kitumike kwa watoto, vijana na wananchi wa Malawi kwa ujumla amesema Balozi Humphre Polepole.

Imetolewa na,

Ubalozi wa Tanzania Lilongwe, Malawi