Na. James K. Mwanamyoto-Dar es Salaam
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Jenista Mhagama amesema Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi, na Utamaduni (UNESCO) linatambua kuwa Tanzania kupitia Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa ina hifadhi kubwa ya nyaraka za utawala wa kijerumani ambazo hazipatikani sehemu nyingine yoyote duniani.

Waziri Jenista amesema hayo jijini Dar es Salaam alipokitembelea Kituo cha Kumbukumbu Kanda ya Mashariki na kujionea nyaraka hizo za kijerumani pamoja na taarifa hiyo ya UNESCO inayoitambua Tanzania kuwa na kumbukumbu za nyaraka muhimu za utawala wa Kijerumani.

Mhe. Jenista amesema, kitendo cha UNESCO kugundua kuwa Tanzania ina nyaraka muhimu za utawala wa kijerumani zisizopatikana sehemu nyingine duniani, ni jambo la kujivunia kama nchi kwani Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa imefanikiwa kuhifadhi nyaraka hizo ambazo zinalipa taifa heshima kubwa duniani ya utunzaji mzuri wa kumbukumbu za kihistoria.

“Sasa ni wakati muafaka na fursa adhimu ya kuzitangaza nyaraka hizi muhimu za kijerumani tulizozihifadhi ambazo zimepewa heshima ya kutambuliwa na UNESCO kama nyaraka muhimu na maalum ambazo hazipatikani mahali pengine duniani, ili ziweze kuwa kivutio kikubwa cha watalii nchini”, Mhe. Jenista amesisitiza.

Waziri Jenista ameongeza kuwa, Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan amefanya kazi kubwa ya kutangaza vivutio vya watalii kupitia Royal Tour, hivyo Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa imuunge mkono kwa kutangaza amali hii ya nyaraka muhimu za utawala wa kijerumani ili kuongeza idadi ya watalii watakaoliongezea taifa kipato cha fedha za kigeni.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Bw. Firimin Msiangi, amesema nyaraka hizo za utawala wa iliyokuwa German East Africa (Tanganyika, Zanzibar, Burundi na Rwanda) ambayo Makao Makuu yake yalikuwa Dar es Salaam-Tanganyika ziliingizwa kwenye rejesta ya UNESCO ya mwaka 1997 ya Kumbukumbu ya Dunia na kutambuliwa rasmi kama sehemu ya Kumbukumbu ya Dunia (Memory of the World).

Aidha, Bw. Msiangi ameongeza kuwa idara yake ni ya huduma za nyaraka ambazo hazitumiki kwenye matumizi ya kawaida ya kila siku lakini zimethibitika kuwa na thamani endelevu katika historia ya taifa kwenye masuala ya kiutawala, kisheria, kiuchumi na kitafiti.

Akizungumzia mchakato wa upatikanaji wa nyaraka nyingine zinazohifadhiwa, Bw. Msiangi amesema sheria inaitaka Idara yake kufanya uchambuzi wa nyaraka kwenye Wizara, Idara zinazojitegemea, Wakala za Serikali, Mamlaka na Taasisi nyingine za Umma ili kuzihifadhi katika eneo salama kwa sababu idara yake ina wataalam na vifaa vya vya kuifadhia.

Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa inatekeleza shughuli zake kwa mujibu wa Sheria ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa Na. 3 ya mwaka 2002 na mnamo mwaka 2004 Bunge lilitunga Sheria Sheria Na. 18 ya Mwaka 2004 iliyoiongezea idara hiyo jukumu la Kuhifadhi Nyaraka za Waasisi wa Taifa (Mlm. J.K Nyerere na Sheikh Abeid Amani Karume).