Na Lucas Raphael,Tabora
Miili ya vijana wawili wanaokadiriwa kuwa na umri kati ya miaka 29 na 25  imekutwa imetelekezwa pembezoni mwa barabara kuu inayotoka Tabora kuelekea Kigoma eneo la Kata ya Malolo manispaa ya Tabora baada ya kupingwa na watu wenye hasira kali kwa tuhuma za kuvunja na kuiba.

Kamanda  wa  Polisi mkoa wa Tabora ACP Richard Abwao akitoa Taarifa kwa vyombo vya habari jana ofisini kwake alisema kuwa tukio hilo lilitokea katika kata ya malolo manispaa ya Tabora mkoani hapa

Alisema kwamba taarifa za awali  zinasema vijana hao wanadaiwa kuuawa majira ya usiku wa kuamkia aprili 9 mwaka huu ambapo maiti zao zilikutwa zimetelekezwa majira ya saa 1 na Robo Asubuhi mpembezoni mwa barabara ya Kigoma .

Kamanda huyo wa polisi alisema watu hao walituhumiwa kuusika katika tukio la uhalifu ambalo wanadaiwa kuvamia nyumba  moja wakitaka kufanya uhalifu hali iliyosababisha wananchi kujitokeza na kuanza kuwashambulia hadi kusababisha vifo vyao.

Aidha jeshi la polisi lilifanikiwa kumtambua moja kati ya wawili hao ambao ni Masudi mrisho (29) mkazi wa malolo na mwingine anakadiriwa kuwa na umri wa miaka 25 hakufahamika  jina wala sehemu anakoishi.

Abwao alisema kwamba watu hao walikutwa majeraha makubwa sehemu mbalimbali ya miili yao yaliyosabishwa na kipigo walichokipata .

Hata hivyo kamanda huyo wa polisi mkoa wa Tabora alisema kwamba wanafanya msako mkali kubaini watu walifanya uhalifu huo kwani kitendo cha kujichukulia sheria mkononi ni kosa hivyo itakuwa ni onyo kwa watu wengine wanaojichukulia sheria .

“Ni marufuku kwa wananchi sehemu yoyote mkoani Tabora kujichukulia sheria mkononi na yoyote atakaye bainika kujichukulia sheria mkononi hatambue kufanya hivyo kosa kisheria na sheria haitamuacha mtu salama itamuajibisha kwa kufikisha kwenye vyombo vya sheria ”alisema Abwao.

Aidha kamanda huyo alitoa wito kwa wananchi kuacha kitendo cha kujichukulia sheria mkononi hivyo ni muhimu  watuhumiwa wanapokamatwa wapelekwe kwenye vituo vya polisi salama kwa ajili ya mahojiano ili kubaini watu hao mtandao wao wa uhalifu wanashirikianana kinanani ,wahalifu kutoka maeneo gani  na kufahamu mali zilizoibiwa siku za nyumba .