Urusi ilitangaza siku ya Jumatano kwamba imekamilisha kwa mafanikio jaribio la kwanza la kombora lake jipya la masafa marefu la "Sarmat", silaha ambayo inachukua nafasi ya makombora ya SS-18 "Shetani" na ambayo itakuwa jibu la jeshi la Urusi kwa mpangi wa Marekani wa Global Strike.

RS-28 Sarmat( NATO wanaiita Shetani-2)  ni silaha ya kizazi kipya. Kombora la masafa marefu la nyuklia, la tano la kizazi chake, ambalo halina mfano wake, kulingana na Rais wa Urusi Vladimir Putin.

Kombora hilo lina uwezo wa kuwa na vichwa kadhaa vya nyuklia au vya kawaida ambavyo kila moja hufuata mkondo huru wakati wa kuingia kwenye angahewa, lilifanyiwa majaribio na kurushwa kwa mara ya kwanza Jumatano Aprili 20 katika eneo lililo kaskazini magharibi mwa Urusi.

 Kombora hilo linaaminika kulenga shabaha yake Mashariki ya Mbali ya Urusi, kilomita 5,000 kutoka eneo la kurushia.

Lakini kombora la Sarmat linaweza kwenda zaidi ya kilomita 11,000, uzito wake unazidi tani 200. Silaha "ambayo itahakikisha usalama wa Urusi licha ya vitisho vya nje na ambayo itawafanya wale wanaojaribu kutishia nchi yetu kwa maneno ya kikatili na ya fujo kufikiria mara mbili," Vladimir Putin alisema wakati wa hotuba ya televisheni. 

Kulingana na Bw. Putin, kombora hilo lina uwezo wa "kushinda mifumo yote ya kisasa ya kuzuia ndege".