Na Mary Gwera, Mahakama-Arusha

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewataka Watumishi wote wa Mahakama nchini kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa awamu ya pili ya Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania na Programu ya Uboreshaji wa huduma za Mahakama kwa kuwa na umiliki (ownership) na uelewa wa pamoja kuhusu mipango iliyowekwa ili iweze kufikiwa kwa mafanikio.

Akizungumza  tarehe 04 Aprili, 2022 jijini Arusha wakati akifungua Kikao kazi cha Mapitio ya Mpango Mkakati wa pili wa Mahakama wa 2020/2021-2024/2025 na Mradi wa Uboreshaji wa Huduma za Mahakama awamu ya pili, Jaji Mkuu amesema kuwa ni muhimu kuwa na uelewa wa pamoja katika utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Mahakama.

“Msingi muhimu wa utekelezaji wa Mpango Mkakati wa Mahakama na Programu ya Uboreshaji wa Huduma za Mahakama ni muhimu kila Mmiliki kwanza kuwa na uelewa wa kina, na pili kuwa na uelewa wa pamoja kuhusu mwelekeo wa kimkakati,” amesema Jaji Mkuu.

Amesema kuwa uzoefu wake katika utekelezaji wa Awamu za kwanza za Mpango Mkakati na Programu ya Maboresho umemfundisha kuwa ni wamiliki wachache waliojijengea tabia ya kusoma na kuelewa mwelekeo wa uboreshaji wa huduma za kimahakama kwa kusoma nyaraka muhimu, kuzielewa na kuzitekeleza.

“Tumezoea sana kuwategemea wachache wasome, waelewe na kisha watutafunie walichoelewa. Tumezoea kutegemea cha kuambiwa. Tumezoea kuwategemea tunaowaongoza ndio wasome na waelewe na kisha sisi tutoe maamuzi ya mwisho bila kujua undani wa nyaraka. Hivyo, ni lazima kila Mmiliki asome neno, kwa neno, na kuzielewa nyaraka muhimu zenye kutoa msingi wa uelewa na urahisi wa utekelezaji,” amesisitiza Prof. Juma.

Aliongeza kuwa ni muhimu kwa Wamiliki wa utekelezaji wa Mpango Mkakati kuelewa mantiki na umuhimu ambao Benki ya Dunia kuridhia kuikopesha Serikali ya Tanzania mkopo mkubwa zaidi ya ule wa Awamu ya Kwanza.

Jaji Mkuu, Mhe. Prof. Juma ameongeza kuwa Mradi wa Uboreshaji wa Huduma za Mahakama una umuhimu pia kwa Serikali kwa sababu ni mojawapo ya nyenzo ya kufikia Malengo Makuu yaliyoainishwa kwenye Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025 (Tanzania’s Development Vision 2025).

“Kwa kutambua nafasi muhimu ya Mradi wa Maboresho ya Mahakama katika kufanikisha Malengo ya Dira ya Maendeleo 2025, Serikali ilitafuta mkopo nafuu wa Benki ya Dunia. Maana yake ni kuwa, Serikali ya Tanzania inatambua kuwa  huduma za utoaji haki ni muhimu katika ukuaji wa uchumi, kuondoa umasikini, kuweka mazingira rafiki kwa biashara na uwekezaji, kuweka mazingira ya uwazi; kuweka usawa katika jamii na kulinda amani na utulivu,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Aidha, Mhe. Prof. Juma aliongeza kuwa katika suala ya uboreshaji wa huduma za mbalimbali ni muhimu zaidi kwenda sambamba na dunia ya karne ya 21 ambayo inazingatia zaidi matumizi ya TEHAMA kwa asilimia kubwa.

Naye Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Mustapher Siyani ametoa rai kwa Watumishi wa Mahakama kuendelea kutoa huduma za Mahakama ili wananchi wanaofuata huduma za Mahakama waridhike na huduma zinazotolewa.

“Tunaenda kuanza awamu ya pili ya utekelezaji wa Mradi wa Uboreshaji wa huduma za Mahakama, hakuna budi kuhakikisha kila mmoja wetu anashiriki katika katika hili ili wananchi tunaowahudumia waweze kuridhika na huduma zetu,” amesema Mhe. Siyani.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel amewataka Watumishi wa Mahakama kuwa na mtazamo/fikra chanya ili kufanikisha utekelezaji wa Mpang Mkakati huku  akibainisha mafanikio yaliyofikiwa na Mahakama katika utekelezaji wa Mpango Mkakati wa awamu ya kwanza wa mwaka 2015/2016-2019/2020 ambayo ni pamoja na kuongezeka kuridhika kwa wananchi/wateja wa Mahakama kutokana na utafiti uliofanywa na ‘REPOA’ ambapo inaonyesha kuwa kiwango cha kuridhika kimeongezeka kutoka asilimia 61 mwaka 2015 hadi asilimia 78 kwa mwaka 2019.

“Mafanikio mengine ni pamoja na ujenzi wa miundombinu ya majengo ya Mahakama ikiwemo Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki sita (6), ujenzi wa Mahakama za Hakimu Mkazi tano (5), Mahakama za Wilaya 15 na ujenzi wa Mahakama za Mwanzo 19, kuongezeka kwa asilimia ya maamuzi yanayoingizwa kwenye mtandao kutoka asilimia 0 kwa mwaka 2015 hadi asilimia 80 kwa mwaka 2021,” amesema Mtendaji Mkuu.

Mpango Mkakati wa Pili wa Mahakama (2020-2025) utatekelezwa kwa kiasi kikubwa na nyongeza ya Mkopo wa Benki ya Dunia baada ya kukamilika kwa matumizi ya kwanza ya Dola milioni 65 ambazo Benki ya Dunia iliikopesha Serikali ya Tanzania kwa matumizi ya kuboresha huduma ndani ya Mahakama ya Tanzania.

Kikao kazi hicho kimehusisha jumla ya Washiriki wapatao 240 wakiwemo Majaji, Wasajili wa Mahakama, Watendaji wa Mahakama na baadhi ya Watumishi wa Kada mbalimbali kinalenga katika kufanya mapitio ya Mpango Mkakati wa Mahakama wa awamu ya pili wa mwaka 2020/2021-2024/2025, kuainisha changamoto za utekelezaji wa awamu ya kwanza na kuja na njia bora zaidi zitakazowezesha utekelezaji fasaha.