Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara Ndg Abdulrahman Omar Kinana amepokelewa wilaya ya Mkuranga  tarehe 24 Aprili, 2022 kwa ajili ya ziara mkoa wa Pwani ya uimarishaji uhai wa


chama na kuhamasisha wana-CCM kujitokeza kushiriki uchaguzi wa ndani ya Chama unaoendelea.

Akizungumza na wanachama wa CCM ukumbi wa CCM wilaya ya Mkuranga Ndugu Kinana amewataka wana-CCM kujitokeza kwa wingi kuomba nafasi za uongozi ndani ya Chama katika uchaguzi unaoendelea pamoja na kuwahimiza viongozi wa ngazi zote kuhakikisha uchaguzi unakuwa wa huru, haki na wenye kuzingatia katiba ya CCM na kanuni zake ili kuwapata viongozi waadilifu.

"Viongozi simamieni uchaguzi uwe huru na haki, acheni kubeba wagombea, epukeni dhulma na chukueni hatua kwa kuwakata wale wanaotafuta uongozi au umaarufu kwa fedha. Kwa kuwa tunataka uadilifu nje ya CCM basi ni lazima tuanze kwanza sisi kuwa waadilifu." Amesema Kinana

Kinana amesisitiza "Wana-CCM wanayo haki ya kuchagua na kuchaguliwa lakini haipo haki ya kununua au kununuliwa ili kupata au kutoa uongozi.  Kuna watu huwa hawana habari na chama wala wanachama wakati ambao sio wa chaguzi ajabu wakisikia uchaguzi tu wanaanza kujipitisha kuwasalimu, kugawa fedha na kuwachafua wengine tusiruhusu haya yajitokeze."

Aidha Kinana amesema mahusiano mazuri baina ya CCM na serikali ni chachu ya utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya CCM hali inayoimarisha imani ya wananchi kwa Chama na serikali yao. Pia amewataka viongozi wa CCM kuendeleza utamaduni wa kuwasikiliza wananchi na kuwasilisha changamoto zao serikalini kwa utatuzi. Amehimiza wajibu huo ni walazima kwa sababu ni CCM inayoomba kura na inayopigiwa kura.

Mapema wakati wa Mapokezi Ndg Kinana ameshiriki uzinduzi wa ofisi ya tawi la Mwanambaya kata ya Mipeko wilaya ya Mkuranga ambapo alichangia shilingi milioni tatu kuunga mkono juhudi za Wana-CCM na viongozi wa tawi hilo za kupata mazingira mazuri ya kufanyia shughuli za Chama.

Katika ziara hii viongozi walioshiriki ni pamoja na mwenyeji wake Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Pwani Ndg Ramadhani Maneno, Kamati ya siasa ya mkoa wa Pwani, kamati za siasa za wilaya zote za Mkoa wa Pwani, Mkuu wa Mkoa wa Pwani Ndg Abubakar Kunenge, wakuu wa wilaya zote, watendaji wote, wabunge na madiwani wote wa Mkoa wa Pwani. Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara Ndg Abdulrahman Omar Kinana ameondoka mkoa wa Pwani kuelekea mkoa wa Tanga kuendelea na ziara yake akiwa ameambatana na Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Itikadi na Uenezi Ndg Shaka Hamdu Shaka.