Rais wa Marekani Joe Biden Alhamisi ameliomba bunge la Marekani kuidhinisha msaada wa ziada wa dola bilioni 33 kuisaidia Ukraine kukabiliana na  vikosi vya Russia katika kipindi cha miezi mitano ijayo.

“Kuwekeza katika uhuru wa Ukraine, ni jambo la maana la kufanya,” Biden amesema katika hotuba kwenye White House.

“Hatuishambulii Russia, tunaisadia Ukraine kujihami,” ameongeza.

Muda mfupi kabla ya Biden kueleza mpango huo, White House imesema matumzi hayo mapya yatajumuisha dola bilioni 20 katika msaada mpya wa kijeshi na zana za kijeshi, msaada wa kiuchumi wa dola bilioni 8.5 na dola bilioni 3 kwa ajili ya msaada wa kibinadamu kwa nchi hiyo ambayo Russia iliivamia miezi miwili iliyopita.

Kiwango hicho ni mara mbili zaidi ya dola bilioni 13.6 zilizopitishwa na bunge ambazo tayari zimekwisha tumiwa kwa kusafirisha shehena za silaha kwa Ukraine katika wiki za hivi karibuni.