Na Mwandishi wetu, Morogoro.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu), Mhe. Profesa Joyce Ndalichako, amezindua rasmi miongozo ya tathmini za ulemavu, inayotumiwa na Madaktari na Wataalamu wa Afya wakati wa kufanya Tathmini za Ulemavu uliotokana na ajali na magonjwa yatokanayo na kazi.

Uzinduzi huo umefanyika Jumatatu Machi 14, 2022 mjini Morogoro wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya tathmini za ulemavu uliotokana na ajali na magonjwa yatokanayo na kazi kwa Madaktari na Watoa Huduma ya Afya kutoka Mikoa ya Kanda ya Pwani ambayo ni Mtwara, Lindi, Dar es Salaam, Pwani na Morogoro chini ya uratibu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF).

“Miongozo hii iliyoandaliwa na wataalamu waliobobea imezingatia matakwa ya Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi Sura 263 na Kanuni za Fidia kwa Wafanyakazi za mwaka 2016 na marekebisho yake na itatumika katika mafunzo haya ili kuwajengeeni uwezo wa kufanya tathmini za ulemavu kwa usahihi.” Alisema.

Alisema anaamini kuwa matumizi ya miongozo hii inaongeza ufanisi na urahisi katika kufanya tathmini za ulemavu na kuwezesha WCF kuchakata madai ya fidia kwa wakati.

Akizungumzia mafunzo ya Madaktari na Watoa Huduma ya Afya, Mhe. Profesa Ndalichako alisema ni endelevu, ambapo WCF ilianza zoezi hilo la mafunzo kwa madaktari katika mwaka wa fedha 2015/16. Mpaka sasa, jumla ya madaktari 1,301 kutoka wilaya mbalimbali hapa nchini wameshapatiwa mafunzo.

“WCF imeshafanya mafunzo ya aina hii katika Kanda ya Kati, Kanda ya Ziwa, Kanda ya Kaskazini, Kanda ya Nyanda za juu Kusini na Kanda ya Pwani.” Alifafanua Prof. Ndalichako.

Mhe. Waziri pia alisema uwepo wa WCF ni hatua muafaka katika mazingira ya sasa ambapo Serikali ya Awamu ya Sita, chini ya Uongozi mahiri wa Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inaendelea na kazi ikiwemo ya kujenga uchumi wa viwanda na hivyo kuwa na ongezeko kubwa la maeneo ya uzalishaji linalokwenda sambamba na ongezeko la matukio ya ajali au magonjwa yatokanayo na kazi.

“Katika mazingira haya, jukumu la Mfuko siyo kulipa fidia pekee bali pia kushirikiana na wadau katika kubuni, kukuza na kuendeleza mbinu za kupunguza ama kuzuia kabisa ajali na magonjwa katika maeneo ya kazi.”. Alisema na kuongeza .....Naelekeza WCF iendelee kutoa elimu na mafunzo kwa madaktari, kuhusu tathmini za ulemavu unaotokana na magonjwa na ajali zitokanazo na kazi.

Alisema WCF ina faida kubwa kwa Wafanyakazi, Waajiri na Taifa kwa ujumla kwani hivi sasa wafanyakazi wanauhakika wa kinga ya kipato kutokana na majanga yasababishwayo na ajali, magonjwa au vifo kutokana na kazi, Waajiri nao wanapata muda zaidi wa kushughulikia masuala ya uzalishaji na uendeshaji wa biashara zao kwani Mfuko ndio unaobeba jukumu na gharama pindi mfanyakazi anapoumia, kuugua ama kufariki kutokana na kazi.

Faida nyingine alitaja ni kuongezeka kwa pato la Taifa kutokana na kukua kwa tija na uzalishaji, vilevile utoaji huduma bora kutokana na mahusiano mazuri mahali pa kazi kati ya mwajiri na mwajiriwa.

Awali Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Dkt. John Mduma alisema kuna mabadiliko makubwa sana ya uboreshaji wa mazingira ya uwekezaji na biashara hapa nchini ndani ya kipindi cha Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Katika mabadiliko hayo sisi WCF tunajivunia siku 365 za Mama Samia Suluhu Hassan, kwa uboreshaji wa huduma za Fidia ikiwemo punguzo la kiwango cha uchangiaji kwa sekta binafsi kutoka asilimia 1% hadi 0.6% na punguzo la riba (interest) kwa madeni ya michango ya nyuma, kwa sekta zote kutoka asilimia 10% na kushuka mpaka asilimia 2% tu.” Alifafanua Dkt. Mduma.

Maboresho haya yanalenga kukuza uzalishaji ambapo sasa Waajiri wa Sekta binafsi wamepewa nafuu kubwa ya kuelekeza nguvu katika uzalishaji mali, huku Mfuko ukiendelea kulinda nguvukazi ya Taifa. Hivyo basi, tunaendelea kuwakumbusha Waajiri kutumia fursa hii adhimu, iliyowezeshwa na Serikali sikivu ya Awamu ya Sita. Alisema Dkt. Mduma.