Na: Mwandishi wetu – Dodoma

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu Mhe. Prof. Joyce Ndalichako ametembelea na kukagua maendeleo ya awamu ya pili ya ujenzi wa ofisi yake unaoendelea katika Mji wa Serikali, Mtumba Jijini Dodoma.

Akiwa katika ukaguzi huo, Waziri Ndalichako amesisitiza kuongeza kasi ya ujenzi kwa Mkandarasi SUMA JKT ili kuendana na ratiba iliyotolewa na Serikali kukamilisha ujenzi huo.

“Ni dhamira ya Serikali kuona majengo ya ofisi yanakamilika kwa wakati ili watumishi waweze kukaa na kufanya kazi kwa pamoja hali ambayo itaongeza ufanisi wa utendaji kazi wao na utoaji wa huduma wa ofisi hiyo, hivyo ni vyema mkandarasi akaongeza jitihada katika kukamilisha ujenzi huu,” alisema Ndalichako

Wakati huo huo Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu Mhe. Prof. Joyce Ndalichako ametaka Mkandarasi huyo kuhakikisha wanatekeleza mpango mkakati iliyojiiweka ili ujenzi wa ofisi hiyo ukamilike kwa wakati.

Kwa Upande wake, Mhandisi Ujenzi kutoka SUMA JKT, Capt. Khalfan Mturi ameahidi kutekeleza maelekezo yote yaliyotolewa na mheshimiwa Waziri. Pia alieleza kuwa wamejipanga kuongeza nguvu kazi ili kufanikisha shughuli hiyo ya ujenzi.

Katika ziara hiyo Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu Mhe. Prof. Joyce Ndalichako, Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu) Mhe. Prof. Jamal Katundu, Wakurungenzi wa Idara na Vitengo pamoja na Wakuu wa Taasisi zilizopo chini ya Ofisi hiyo.