Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Sensa ya watu ba Makazi Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa amewataka watendaji wanaosimamia kuwa wawazi katika majukumu yao ili kuendana na Azma ya Serikali zote mbili kwa kuwaletea maendeleo wananchi wake.


Mhe. Majaliwa ambae ni Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ametoa agizo hilo alipokuwa akiendesha Kikao cha Nne cha Kamati hiyo kilichofanyika Ukumbi wa Hotel Verde Mtoni Jijini Zanzibar.

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Awamu ya Nane zimeweka utaratibu wa kuweka wazi matumizi kwa lengo la kudhibiti matumizi katika Serikali.

Aidha Mhe Majaaliwa amesema ni vyema kwa matumizi ya vifaa vitakavyotumika kwa ajili ya Zoezi la Sensa ya watu na Makazi yafanywe kwa kufata utaratibu ili kutumia fedha kwa mujibu wa sheria za manunuzi zilizopo nchini.

Nae Mwenyekiti Mwenza wa kamati ya kitaifa ya Sensa ya watu na makazi Mhe. Hemed Suleiman Abdulla ambae pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amezitaka Wizara husika kuacha Muhali katika kutoa nafasi za ajira na kueleza kuwa ni vyema kuzingatia vigezo vinavyohitajika katika kupatikana watumishi hao.

Amesema Serikali haitoridhia kuona baadhi ya watumishi wake kuvuruga zoezi hilo kwa Maslahi yao binafsi ambapo hatua za kisheria zitachukuliwa kwa yoyote atakaevuruga zoezi hilo.

Hata hivyo Mhe Hemed amesema Serikali ina matumaini Makubwa kwa zoezi hilo hivyo ni vyema kila mmoja kuhakikisha anawajibika ipasavyo ili liweze kukamilika kwa Maslahi ya Taifa.

Nao Makamisaa wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022 wamesema Makarani watakaotumika kusimamia zoezi hilo watachukuliwa kwa mujibu wa maeneo yao ya makazi ili kuhakikisha zoezi hilo linakamilika kwa urahisi na kwa wakati uliopangwa.