WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Innocent Bashungwa amesema wanafunzi waliomaliza Kidato cha Nne mwaka 2021 wanayo nafasi ya kubadili machaguo ya tahasusi (Combination) na kozi mbalimbali wanazohitaji kusoma kulingana na ufaulu wao.

Kauli hiyo ameitoa  Machi  29,2022 Jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari Waziri Bashungwa amesema, hatua hiyo inatokana na baadhi ya wanafunzi waliohitimu Kidato cha Nne kutokujaza fomu (Selfom) kwa uhakika wakati wanachagua combination zau kozi zao kutokana na kutokuwa na uhakika wa ufaulu katika masomo yao.

“Ofisi ya Rais -TAMISEMI imekamilisha zoezi la awali la kuingiza kwenye kanzi data taarifa zilizo kwenye fomu za mwanafunzi kama zilivyojazwa na wanafunzi wakiwa shuleni, hii inazoa nafasi kwa wanafunzi kuweza kufanya mabadiliko ya machaguo yao” amesema Bashungwa

Aidha amesema kuwa Serikali imetoa fursa kwa wahitimu wa Kidato cha Nne kubadili machaguo yao ili kutoa nafasi zaidi kwa mwanafunzi kusoma tahasusi au kozi itakayomwandaa kuwa na utaalam ambao unaendana na machaguo yake hapo baadae.

“Amewataka wazazi kushiriki kikamilifu na kukubaliana na mwanafunzi katika zoezi hili ili pasiwepo na malalamaiko yoyote ya mwanafunzi kuwa amepangiwa machaguo ambayo hakuyachagua hapo baadae” amesema Waziri Bashungwa

Hata hivyo amefafanua kuwa zoezi la kubadilisha tahasusi kwa mwanafunzi linafanyika kwa utaratibu wa kuingia kwenye mfumo wa uchaguzi wa wanafunzi (student Selection MIS) kupitia kiunganishi cha selform.tamisemi.go.tz kwa kutumia namba ya mtihani.

Waziri Bashungwa ametoa ushauri kwa wazazi,walezi na wanfunzi kuendelea kutumia dawati la huduma kwa wateja kupitia barua pepe helpdesk@tamisemi.go.tz au na kituo cha huduma kwa wateja kwa simu namba +255 262 160 20 na +255 735 260 210 au fika katika ofisi za Mamlaka za Serikali za Mitaa.