Mwandishi Wetu- Dodoma
Serikali ya Tanzania imewakaribisha wawekezaji wa masuala ya kilimo kuwekeza nchini ili kuongeza mnyororo wa thamani wa mazao ya kilimo na kuimarisha lishe kwa wananchi na kuinua pato la Taifa.
 
Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, na Uratibu Mhe. Balozi. Dkt Pindi Chana  alipokutana na kufanya mazungumzo na  Mwakilishi wa Shirika la Chakula la Umoja wa Mataifa (WFP) Tanzania Bi. Sarah Gibson  na Mkurugenzi wa Shirika hilo Kanda ya Kusini wa Afrika Dkt. Manghestab Haile Ofsini kwake Bungeni Jijini Dodoma.
 
Akileleza baadhi ya masuala yaliyoafikiwa ni pamoja na kuboresha suala la lishe kwa wananchi licha ya uzalishaji mkubwa wa chakula katika maeneo mbalimbali hatua itakayoboresha afya na kuepuka utapiamlo huku akisema kuwa Tanzania ni sehemu salama kwa ajili ya kufanya uwekezaji katika nyanja ya kilimo.
 
“Tunaposhirikiana na WFP chini ya Rais wetu mpendwa Mhe. Samia Suluhu Hassan Tanzania ni eneo sahihi kabisa katika uzalishaji wa chakula tumekuwa  tukizalisha chakula cha kutosha na tumekuwa mfano ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Nchi za SADC na tumekuwa tukipeleka chakula nje ya Nchi,”alisema Mhe. Pindi Chana.
 
Pia Waziri Pindi alieleza kwamba wamefikia makubaliano ya kushirikiana katika masuala ya maafa pindi yanapojitokeza kwani yamekuwa yakisababisha maafa kwa raia kama vifo, mali zao kuharibiwa  na miundo mbinu.
 
Vilevile Mhe. Pindi alibainisha kwamba wamekubaliana kuboresha sula la kilimo kuendana na teknolojia iliyopo sasa na matumizi sahihi ya pembejeo pamoja na ushirikishwaji wa vijana katika uzalishaji wa chakula, masoko na kuongeza mnyororo wa thamani wa mazao ya kilimo.
 
“Katika majadiliano tumezungumzia suala zina la kilimo kuna matumizi ya vitendea kazi vya kisasa, ushirikishwaji wa vijana maana idadi kubwa ya umri wa watu ni vijana na sasa tunaelekea sensa ya watu na makazi mwaka huu asilimia 50 kwahiyo ni jinsi gani tunahamasisha  vijana katika uzalishaji wa chakula na kuongeza thamani yake,” alieleza  Mhe. Pindi.
 
Katika hatua nyingine aliwahakikisha kwamba kuelekea Bunge la bajeti ijayo sekta ya kilimo imepewa kipaumbele kuhakikisha kinaleta tija na kuona namna ya kushrikiana na WFP kuboresha eneo hilo muhimu la chakula.
 
Kwa upande wake Mwakilishi wa  Shirika la Chakula la Umoja wa Mataifa nchini Tanzania  ( WFP) Bi. Sarah Gibson aliipongeza Serikali ya Tanzania kwa namna ambavyo imekuwa mstari wa mbele kuhakikisha Taifa  linakuwa na chakula cha kutosha na chenye ubora akisisitiza kuendeleza uhusiano baina Tanzania na Shirika hilo.
Naye Mkurugenzi wa Shirika la Chakula la Umoja wa Mataifa (WFP) wa Kanda ya Kusini mwa Afrika Dkt. Manghestab Haile aliiahidi Serikali ya Tanzania kuendelea kushirikiana na sekta binafsi, kuimarisha masoko na lishe bora kwa raia wake.
 
Akihitimisha Mkurugenzi Msaidizi wa Menejimenti ya Maafa kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu Bw.Charles Msangi alishukuru ugeni huo wa wadau wa maendeleo na kusema kwamba utasaidia kutatua changamoto zilizopo katika usimamizi wa maafa.