Kansela wa Ujerumani, Olaf Scholz amerudia kusisitiza kwamba Jumuia ya Kujihami ya NATO haitoingilia kijeshi nchini Ukraine baada ya Rais wa nchi hiyo, Volodymyr Zelensky kuliomba bunge la Ujerumani kusaidia kuilinda nchi yake dhidi ya uvamizi wa Urusi. 

Scholz amemshukuru Zelensky kwa maneno yake mazuri kwa Bunge la Ujerumani, Bundestag leo asubuhi. 

Hata hiyo, Scholz amesema jambo moja linapaswa kuwekwa wazi kwamba NATO haitoingilia kati kijeshi katika vita vya Ukraine. Wakati huo huo, Katibu Mkuu wa NATO, Jens Stoltenberg amesema leo kuwa jumuia hiyo imeazimia kuzuia vita nchini Ukraine visiongezeke zaidi. 

Akizungumza na waandishi habari katika mkutano wa pamoja na Scholz mjini Berlin, Stoltenberg amesema NATO ina jukumu la kuuzuia mzozo huo usizidi kuongezeka. 

Aidha, amepongeza juhudi za Scholz za kutafuta suluhu ya kidiplomasia katika vita hivyo, ikiwemo kuwasiliana moja kwa moja na Rais wa Urusi, Vladimir Putin.