Mamlaka katika mji wa bandari uliozingirwa nchini Ukraine, Mariupol imesema jeshi la Urusi limeishambulia shule ya sanaa ya mji huo, eneo ambalo lilikuwa likiwahifadhi takribani watu 400 waliopoteza makazi.

Imesema jengo la shule limeteketezwa kabisa na kwamba watu hao wanaweza kuwa wamesalia chini ya kifusi, ingawa bado hakujawa na taarifa za vifo. 

Jumatano iliyopita majeshi hayo pia yalidaiwa kulishambulia eneo la kuwahifadhi watu.Kwa tukio hilo la awali, mamlaka ilisema watu 130 waliokolewa, lakini wengi wao walibaki katika mabaki ya jengo. 

Mariupol, mji wa bandari ya kimkakati katika Bahari ya Atov umezungukwa na vikosi vya Urusi, wakikata nishati ya umeme na maji huku ukikabiliwa na mashambulizi ya mabomu.

Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelenskyy amesema mzingiro wa Mariupol utaingia katika rekodi za kihistoria, kutokana na kile alichodai uhalifu wa kivita ambao umefanywa na vikosi vya Urusi.