WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ana dhamira ya dhati kuhakikisha kila Mtanzania anapata fursa sawa ya kufanya biashara katika mazingira bora na rafiki kwa biashara ili kukuza uchumi.

Waziri Mkuu ameyasema hayo jana(Jumatano, Machi 9, 2022) wakati alipotembelea mradi wa ujenzi wa Soko la Wafanyabiashara Wadogo (Machinga Complex) lililoko barabara ya Bahi Mkoani Dodoma na kusema ameridhishwa na ujenzi wa soko hilo.

“Lengo la maboresho haya kwa wafanyabiashara wadogo ni kutaka kutengeneza fursa zaidi kwa kuwa na maeneo salama yanayotambulika na yanayoweza kutumika na taasisi za kifedha kutoa mikopo na fursa nyingine za kiuchumi.”

Waziri Mkuu ameupongeza uongozi wa Mkoa wa Dodoma kwa ubunifu na kuwataka viongozi hao waendelee kusimamia mradi huo na kuukamilisha kwa wakati pamoja na kubuni maeneo mengine ya nje ya mji Ili kukuza maeneo mengi zaidi kibiashara katika mkoa huo.

AIdha, Waziri Mkuu amewataka wafanyabiashara wadogo wa mkoa huo wafuate utaratibu utakaowekwa na mkoa huo mara baada ya ujenzi kukamilika. “Serikali imeendelea kutafuta fursa za kifedha kwa wafanyabiashara wadogo, hivyo jipangeni kutumia fursa hizo kwa uaminifu.”

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais- (TAMISEMI), Innocent Bashungwa amesema Mkoa wa Dodoma umefanya kazi kubwa ya kutekeleza mradi rafiki kwa wamachinga wa mkoa huo. “Niwasihi wakuu wa mikoa mingine kuiga mfano huu kwa kujenga miradi ya kuwapanga machinga kulingana na mazingira yaliyo katika mikoa yenu.”

Naye, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Profesa Joyce Ndalichako ametumia fursa hiyo kutoa wito kwa vijana kuendelea kutumia fursa mbalimbali zinazotolewa na Serikali ili waweze kujikwamua kiuchumi.

Awali, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Anthony Mtaka amesema mradi huo utakapokamilika mwezi mei, machinga wote walioko katika maeneo ya jiji la Dodoma watahamishiwa kwenye eneo hilo rasmi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma, Bw. Joseph Mafuru amesema mradi huo unatarajiwa kukamilika Mei mwaka huu na utagharimu shilingi bilioni 7.5 hadi kukamilika kwa awamu zote huku akisema kuwa mradi huo utakuwa na manufaa makubwa kwani utaiwezesha Halmashauri kukusanya shilingi bilioni 1.1 kwa mwaka.

Nao, wafanyabiashara ndogondogo ambao ndio wanufaika wa mradi huo wameishukuru Serikali kwa kuwezesha ujenzi wa mradi huo na kwamba wako tayari kupokea maelekezo ya mkoa na kufanya biashara katika eneo hilo.