Na Mwandishi Wetu, Dubai
WAZIRI wa Kilimo, Hussein Bashe amesema kuwa Tanzania ipo tayari kushirikiana na kampuni kubwa duniani kuwekeza kwenye kilimo ili kukiongezea thamani na kuhakikisha usalama wa chakula unazingatiwa.

Akihutubia kwenye Maonesho ya Biashara Kimataifa yanayoendelea nchini Dubai (Dubai Expo), Bashe alibainisha kuwa Tanzania ina ardhi kubwa yenye rutuba kwa uwekezaji wa kilimo huku mazingira ya uwekezaji yakiwa ya kuvutia uwekezaji katika kila aina ya kilimo.

Alisema, kwa sasa nchi inatafuta wawekezaji wa kimkakati ambao watasaidia uwekezaji wenye tija kwa Tanzania na dunia kwa ujumla hasa ikizingatiwa kuwa kwa miaka ijayo Afrika ndiyo itakuwa chanzo kikubwa cha chakula.

“Tanzania inawapenda na kuwatambua wawekezaji katika sekta zote hasa za kilimo kwa kuwa ni sekta ambayo ipo na itaendelea kuwepo miaka yote kwa kuwa chakula ni kitu muhimu ambacho bado kinahitajika kwa mustakabali wa mwanadamu kuendelea kuishi, labda wanasayansi waje na utaalamu wa kuweka chipu mwilini ili mtu akiamka asisikie njaa” alisema Bashe.

Alisema uamuzi wa Rais Samia Suluhu Hassan kupunguza riba za benki hadi chini ya asilimia 10 kunawavutia wawekezaji zaidi wa ndani na nje ya nchi, hivyo ni fursa kubwa kwa wawekezaji hao kujikita kwenye kilimo kwa kuwa mazingira ni rafiki zaidi.

Alisema Tanzania inajulikana kimataifa kwa uzalishaji wa mazao ya kilimo na ina vyeti vya utambulisho wa kimataifa ambavyo vinawawezesha wawekezaji hao kuuza bidhaa kimataifa kutoka Tanzania.

Alisema nchi ina vituo vingi vya utafiti wa kilimo ambavyo vinafanya utafiti wa aina ya mazao yanayopaswa  kulimwa katika eneo husika, hivyo wawekezaji watanufaika.

Bashe alisema Tanzania ina nguvu kazi ya kutosha ya kufanya kazi kwenye mazingira yoyote ya uwekezaji huku pia kukiwa na motisha nyingi kwa ajili ya wawekezaji na kwamba nchi ipo tayari kufanya kazi na wawekezaji katika kilimo hasa ikizingatiwa ardhi ipo ya kutosha.

Alitolea mfano wa kampuni ya AVOAAFRIKA ambayo imesafirisha kontena zaidi ya 200 za parachichi kutoka Tanzania na kubainisha kwa sasa kilimo ni biashara na siyo sehemu tu ya kujipatia mlo.

Alisema Dubai inachukuliwa kati ya sehemu muhimu kwa kuuza mazao ya kilimo kutoka Tanzania.

Alisema kwa upande wa kilimo cha matunda na mbogamboga Tanzania inasifika kwa kuwa na uwezo wa kuzalisha aina zote za matunda na mbogamboga huku fursa zikiwa nyingi za kuuza ndani na nje ya nchi huku akifafanua zaidi kuwa hapa nchini kuna mazingira mazuri ya kilimo cha umwagiliaji.

Alisema kuwa licha ya kuwaalika wawekezaji kutoka nje, pia wizara yake inawathamini na kuwaendeleza wakulima wadogowadogo na imeshawawezesha kunufaika na mikopo ya aina mbalimbali kama ilivyo kwa wajasiriamali wengine wadogowadogo.