Bunge la Tanzania limeishauri Serikali kuangalia uwezekano wa Daraja la Tanzanite, kuwa la kulipia (Toll Bridge) ili isaidie kurejesha fedha za mkopo zilizotumiwa kujenga daraja hilo, kama ambavyo inafanyika kwa Daraja la Kigamboni.

Daraja la Tanzanite jijini Dar es Salaam lenye urefu 1.03km na barabara unganishi 5.2km limejengwa kwa gharama ya dola za Marekani milioni 107.4 (Shilingi bilioni 243.8).

Fedha za ujenzi wa daraja hilo ni mkopo wa masharti nafuu kutoka Jamhuri ya Korea kupitia Mfuko wa Ushirikiano wa Maendeleo ya Kiuchumi (EDCF) na Serikali ya Tanzania.

Daraja hilo ambalo pamoja na kurahisisha usafiri na usafirishaji na kutumika kama kivutio cha utalii linatarajiwa kudumu kwa muda wa miaka 100.

Hata hivyo, wakati Bunge likipitisha ushauri huo, Mbunge wa Kigamboni, Dkt. Faustine Ndugulile amesema wananchi wamemtuma kuwasilisha serikalini kilio chao wakiomba kuondolewa tozo kwenye Daraja la Kigamboni.