Na. Saidina Msangi na Farida Ramadhani, WFM, Dodoma
Serikali imesema imewalipa wakulima wa korosho wilayani Tandahimba mkoani Mtwara zaidi ya shilingi bilioni 332.7 zikiwa ni bima ya amana kwa wateja wa iliyokuwa Benki ya Covenant ambayo ilifilisiwa na Serikali kwa mujibu wa sheria.

Hayo yameelezwa bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Hamad Hassan Chande (Mb), alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Tandahimba Mheshimiwa Katani Ahmed Katani, aliyetaka kujua ni lini Serikali itawalipa wakulima wa korosho waliofanya biashara msimu wa mwaka 2017/2018 na iliyokuwa Benki ya Covenant iliyofungwa kabla ya wakulima hawajatoa fedha zao.

“Hadi kufikia mwezi Desemba 2021, jumla ya shilingi 332,715,894.00 zimeshalipwa kwa Wakulima wa Korosho 1,078 kati ya Wakulima 1,346 wa Wilaya ya Tandahimba waliokuwa na amana katika Benki ya Covenant, ikiwa ni asilimia 98 ya kiasi cha shilingi 337,992,095.00 zilizotengwa kwa ajili ya kulipa fidia katika kituo cha Tandahimba,” alisema Mhe. Chande.

Mheshimiwa Chande alisema kuwa kuanzia mwezi Machi mwaka 2018, Bodi ya Bima ya Amana ilianza zoezi la kulipa fidia ya bima ya amana ya kiasi kisichozidi shilingi 1,500,000 kwa wateja waliostahili kulipwa bima hiyo wakiwemo wakulima wa korosho wa Tandahimba na kuwataka wateja ambao hawajachukua fedha zao za bima wafanye hivyo kwani zoezi la ulipaji bado linaendelea.

Mhe. Chande alisema kuwa Benki Kuu ya Tanzania iliifutia leseni iliyokuwa Benki ya Covenant (Covenant Bank for Women (T) Limited) mnamo tarehe 4 Januari 2018 kwa mujibu wa Sheria ya Mabenki na Taasisi za Fedha ya mwaka 2006 na kuteua Bodi ya Bima ya Amana (Deposit Insurance Board – DIB) kuwa mfilisi wa Benki hiyo.

Alieleza kuwa Bodi ya Bima ya Amana inaendelea na zoezi la ufilisi wa Benki hiyo kwa kukusanya mali na madeni ili kupata fedha za kuwalipa wateja waliokuwa na amana zinazozidi shilingi 1,500,000/= ambapo kwa mujibu wa sheria na taratibu za ufilisi kiasi kitakacholipwa kitategemea fedha zitakazopatikana kutokana na kuuza mali za Benki hiyo.