Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Mauritius zimesaini Mkataba wa Jumla (General Framework Agreement – GFA)

Mkataba huo umesainiwa na Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Mauritius mwenye makazi yake Harare Zimbabwe Mhe. Prof. Emmanuel Mbennah pamoja na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Kikanda na Biashara za Kimataifa ya nchini Mauritius Mhe. Balozi Haymandoyal Dillum na kushuhudiwa na Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Kikanda na Biashara za Kimataifa Mhe. Alan Ganoo  

Mkataba huo pamoja na mambo mengine utaimarisha uhusiano wa kiuchumi, kisayansi na kiutamaduni. Mkataba huo pia utaanzisha Tume ya Pamoja ya Kudumu baina ya Nchi itakayokuwa ikifuatilia utekelezaji wa masuala mbalimbli kuhusu ushirikiano wa Tanzania na Mauritius. Hafla ya Uwekaji saini ilihudhuriwa pia na Viongozi wa Serikali na Taasisi kutoka Sekta Binafsi.

Aidha, kwa nyakati tofauti Balozi Mbennah alikutana kwa mazungumzo na Waziri mwenye dhamana na masuala ya Biashara Mhe. Soodesh Satkam Callichurn na Waziri mwenye dhamana na masuala ya Viwanda Mhe. Soomilduth Bholah. 

Mazungumzo na viongozi hao yalijikita katika utekelezaji wa Diplomasia ya Uchumi ili Tanzania na Mauritius ziweze kunufaika na fursa zilizopo katika Nchi hizo.