Tanzania na Morocco zimekubaliana kuimarisha ushirikiano katika nyanja za biashara na uwekezaji, elimu, utalii, uwezeshaji wa kiuchumi kwa wanawake na vijana.

Makubaliano hayo yamefikiwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula (Mb) pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje wa Morocco Bw. Nasser Bourita walipofanya mkutano wa kwa njia ya mtandao. Balozi Mulamula ameshiriki katika mkutano huo akiwa katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

“Tumezungumzia masuala ya kuimarisha uhusiano wetu baina ya Tanzania na Morocco na tumepitia makubaliano yaliyofikiwa wakati wa ziara ya Mfalme wa Morocco alipotembelea Tanzania mwaka 2016 pamoja na kuangalia mikataba mbalimbali iliyotiwa saini wakati wa ziara ya Mfalme wa Morocco ……… laikini pia tumejadili umuhimu wa kuwa na tume ya pamoja ya ushirikiano,” Amesema Balozi Mulamula.

Katika mkutano huo, viongozi hao wamejadili na kukubaliana kuimarisha ushirikiano wa karibu katika sekta za biashara na uwekezaji, utalii, elimu hasa katika kuongeza idadi ya ufadhili wa masomo kwa watanzania kutoka wanafunzi 30 hadi 50.

“Morocco ni nchi inayopata watalii wengi, hivyo tumekubaliana kushirikian kwa karibu zaidi ili kuweza kupata uzoefu ni njia gani wanatumia katika kukuza sekta ya utalii,” ameongeza Balozi Mulamula.

Katika tukio jingine, Balozi Mulamula amekutana na kufanya mazungumzo na Kaimu Balozi wa Oman nchini Dkt. Salim Saif Al Harbi katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.

Mazungumzo ya viongozi hao yamelenga kujadilia masuala mbalimbali ya kuendeleza na kuimarisha ushirikiano uliopo baina ya Serikali ya Tanzania na Oman.