Na Mwamvua Mwinyi Pwani
MSEMAJI Mkuu wa Serikali , Gerson Msigwa amethibitisha Kuwa nchi haiwezi kuingia Gizani kama baadhi ya watu wanavyodai ,kwani kinachofanyika ni maboresho na matengenezo ya kawaida ikiwemo kituo Cha umeme wa gas Songosongo.


Aidha ameeleza, hakuna mradi mikubwa ya kimkakati utakaokwama Wala uliokwama na yote inaendelea vizuri huku wakandarasi wakiwa kazini.


Akizungumzia utekelezaji wa miradi mbalimbali inayotekelezwa na Serikali ya awamu ya sita,kwa waandishi wa habari Mkoani Pwani, Msigwa alisema, shirika la umeme (TANESCO) linafanya maboresho ya kawaida na kuwepo kwa mgao ili kuhakikisha upatikanaji wa umeme nchini unaongezeka.


“Watu waache kujaza wengine maneno ya uzushi,kwani maboresho haya ni ya kawaida na nchi haiwezi kuingia Gizani”alisisitiza Msigwa.
 
Msigwa alisema kuwa kutokana na hali ya upungufu wa mvua umesababisha vyanzo vya kuzalishia umeme maji kupungua hivyo kusababisha mgao ambao lengo ni kufanya maboresho.
 
“Changamoto hii ni kawaida hivyo wakati wa maboresho hayo yanayofanyika Songosongo itasaidia hali kurejea kama kawaida na maboresho hayo hayatafanya nchi kuingia gizani,” alisema Msigwa.
 
Alisema kutokana na uboreshaji huo Watanzania wasiwe na hofu juu ya hali hiyo kwani lengo la Tanesco ni kuhakikisha umeme unapatikana wa kutosha.
 
“Kuanzia hiyo Februari Mosi ni kuboresha visima vya gesi vilivyopo Songosongo hivyo wananchi waondoe hofu juu ya zoezi hilo,” alisema Msigwa.


Pamoja na hayo, Msigwa alisema, ipo miradi mikubwa ya kimkakati Mkoa wa Pwani ikiwemo Bwawa la kufua umeme la Mwalimu Nyerere -Stigo lililopo Rufiji ambapo ujenzi umefikia asilimia 55,Mradi mwingine ni reli ya kisasa (SGR ) uliofikia asilimia 95.


Alieleza kwamba, Serikali inahakikisha miradi inaenda vizuri , na haijashindwa kuwalipa wakandarasi na wakandarasi hao wanaendelea kulipwa.


Msigwa alifafanua hadi sasa Serikali imeshatoa fedha kwa wakandarasi na kazi inaendelea.


Kuhusu umeme alisema kwa mkoa huo mradi wa REA II vijiji 89 vitafikiwa na kupitia mradi wa Ujazilizi Bilioni 5.5 zimetengwa , Bilioni 12 pia imetumika na  miradi 96 imeshakamilika.
Alieleza, Pato la mkoa limekua na kufikia Tirilioni 2.728 kwa mwaka 2019 .


Msigwa akizungumza juu ya fedha za Uviko19 alibainisha, mkoa wa Pwani ulipelekewa Bilioni 16 , ujenzi wa madarasa 422,vituo shikizi vipya 37 na shule mpya za Sekondari 11.


Fedha za elimu bila ya malipo imepelekwa Bilioni 5 na kusema Serikali inaendelea kuweka Mazingira bora kwenye sekta ya elimu.


Akizungumzia sekta ya viwanda aliipongeza mkoa wa Pwani kwa kuwa ukanda wa viwanda,ambapo hadi sasa una jumla ya viwanda 1,453 kati ya hivyo vikubwa 87, vya kati 177 na vidogo 1,057 na umetenga hekta 53.16 kwa ajili ya viwanda.


Upande wa dawa imefikia asilimia 89.5 na Serikali imeanzisha maduka ya dawa ili kurahisisha upatikanaji wa dawa.


Msigwa alikemea Zahanati na vituo vya afya wilayani Kisarawe na maeneo mengine, vinavyofungwa kabla ya wakati na kukemea watumishi wa afya wanaoshindwa kutoa huduma bora kwa wananchi .


Akizungumzia barabara ya Makofia-Mlandizi Msigwa alieleza, ipo Katika utekelezaji na Sasa inafanyiwa upembuzi yakinifu hivyo wananchi wavute subira.