Na Mwandishi wetu, Roma
Wawekezaji zaidi ya 140 kutoka Italia wamewekeza katika miradi mbalimbali nchini Tanzania

Takwimu hizo zimetolewa na Naibu Waziri Wizara ya Madini, Prof. Shukrani Manya alipokuwa akifungua jukwaa la biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Italia lililofanyika jana Jijini Roma, Italia.

Prof. Manya amasema kuwa miradi hiyo inathamani ya Shilingi bilioni 5 inayotoa ajira kwa watanzania zaidi ya 4000.

“Jukwa hili tunataka liendelee kuwa sababu ya kuchagiza uwekezaji mwingine kutoka Italia kwa kutumia teknolojia waliyonayo, kwa kutumia utalaamu walionao wa ‘designing’…….na sasa waone kuwa Tanzania ni sehemu salama ya kuwekeza na Tanzania inaendelea kuweka mazingia wezeshe ya kukuza sekta ya uwekezaji na biashara,” Amesema Prof. Manya

Ameongeza kuwa kupitia jukwaa la biashara na uwekezaji biashara na uwekezaji utaendelea kuongezeka na kuongeza zaidi na hasa katika maeneo ambayo tumawaeleza hapa kupitia jukwaa hili.

Kwa upande wake Balozi wa Tanzania Nchini Italia, Mhe. Mahmoud Thabiti Kombo amesema kuwa kufanyika kwa kongamano hili la biashara na uwekezaji lengo lake kubwa ni kuwavutia wafanyabiashara na wewekezaji wa sekta mbalimbali kutoka Italia kuwekeza zaidi Tanzania.

“mwitukio ni mkubwa na tumeitikiwa na jumuiya za kibiashara na wafanyabiashara na wawekezaji zaidi ya 250 kutoka nchi zote mbili wameshiriki katika kongamano hili,” amesema Balozi Kombo

Balozi Kombo ameongeza kuwa, Wafanyabiashara kutoka italia ni wabobezi katika sekta ya madini lakini pia katika utalii hivyo ni matumanini yake kuwa mara baada ya kumalizika kwa kongamano hilo wawekezaji na wafanyabiashara kutoka Italia wataongezeka zaidi Tanzania.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama Wawekezaji katika Hoteli Zanzibar, Bw. Paulo Rosso amewasihi wawekezaji kutoka Italia kuwekeza kwa wingi Tanzania kwa kuwa mazingira ya biashara na uwekezaji ni tulivu na salama.

“Tanzania ni sehemu salama kuwekeza…..nawahakikishia mimi nimewekeza Tanzania na ninaona ni sehemu salama ya kuwekeza karibuni sana kuwekeza kwa maendeleo ya Tanzania na Italia,” amesema Bw. Rosso

Aidha, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB Abdulmajid Nsekela amewahakikishia wafanyabiashara na wawekezaji walioshiriki katika jukwaa hilo kuwa CRDB ipo tayari kutoa mikopo kwa watakao kuwa tayari kuwekeza Tanzania.

“Nawahakikishia kuwa Benki ya CRDB itawawezesha mikopo ya kuwekeza katika sekta mbalimbali hivyo msiwe na wasiwasi kuhusu mitaji ya kuwekeza ipo karibuni sana tuijenge Tanzania,” Amesema Bw. Nsekela.

Jukwa hilo la biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Italia limehudhuriwa na Wafanyabiashara na Wawekezaji takribani 250 kutoka nchi zote mbili. Wafanyabiashara na wawekezaji hao ni wa sekta za utalii, kilimo, madini, na ujenzi.

Pamoja na mambo mengine, jukwaa hilo limewawezesha wafanyabiashara na wawekezaji kujadili fursa, uwezekano wa ubia, changamoto zinazokabili mazingira ya biashara na njia ya kuboresha mahusiano ya kibiashara kati ya nchi hizo mbili.

Jukwaa la biashara na uwekezaji kati ya Tanzania na Italia limeandaliwa na Ubalozi wa Tanzania nchini Italia kwa kushirikiana na Kituo cha Taifa cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Mamlaka ya Taifa ya Uwekezaji Zanzibar (ZIPA).