Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Dkt. Selemani Jafo amesema Serikali itaendelea kuunga mkono juhudi za Mashirika yasiyokuwa ya Kiserikali (NGOs) katika shughuli za uhifadhi wa mazingira.

Dkt. Jafo ametoa kauli hiyo  Desemba 17, 2021 wakati akifungua Kongamano la Kukomboa Ardhi iliyochakaa katika Nyanda kame za Tanzania sanjari na Maadhimisho ya miaka 10 ya Shirika la Lead Foundation.

Alisema kuwa kongamano hilo linatoa taswira ya namna gani NGOs zinashiriki kikamilifu katika kusukuma mbele agenda ya mazingira nchini hivyo kuwajengea uelewa kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kulinda na kuhifadhi mazingira.

“Niliwahi kuitisha mkutano na mashirika yanayojihusha na suala zima mazingira na leo najisikia faraja kubwa kuona mashirika haya yanapiga hatua na lengo langu kubwa ni kuona kila mmoja anshiriki katika suala zima la uhifadhi wa mazingira,” alisema.

Aidha Waziri Jafo alisema Serikali itaendelea kusimamia Kampeni Kabambe ya Hifadhi na Usafi wa Mazingira inayowashirikisha wadau mbalimbali wakiwemo wadau kutoka mashirika hayo.

Alisema anafarijika kutokana na Mpango Mkakati wa miaka 10 uliozinduliwa na Lead Foundation ambao unaonesha namna gani linaunga mkono Serikali katika hatua za kutunza na kuhidhi mazingira hususan katika eneo la mabadiliko ya tabianchi linaloikabili dunia.

Kwa upande mwingine alitumia nafasi hiyo kuwa kutoa rai kwa wanachi kutumia kipindi hiki cha masika kupanda miti kwa wingi na kuitunza ili kukabiliana na ukame ambao huleta athari mbalimbali za kijamii.

Aliwaelekeza wakuu wa mikoa na wilaya kusimamia vizuri zoezi hilo na kuhakikisha misitu haichomwi ovyo ili kuepusha athari za mabadiliko ya tabianchi zinazochangia kukosekana kwa mvua.

Akitoa shukrani, Mwanzilishi wa Shirika la Lead Foundation, Askofu mstaafu Dkt. Simon Chiwanga alisema kazi ya ukumbozi wa mazingira inafanywa kwa namna mbili ambazo ni kuelimisha na kumbadilisha mtu fikra.

Alisema kupitia uwasilisha wa elimu ya mazingira unaofanywa na Waziri Jafo Dkt. Jafo ni wa kipekee na unaweza kubadilisha fikra za wananchi kuona umuhimu wa kushiriki kuhifadhi mazingira.

“Nafurahia sana uwepo wako hapa mheshimiwa waziri na hiyo ‘passion’, hiyo huruma na upendo ulio nao tunamuomba Mungu akubariki sana,” alisema Askofu mstaafu Chiwanga