Waziri wa Nishati, January Makamba amekutana na kufanya mazungumzo watendaji wa kampuni ya TotalEnergies ambayo hujishughulisha uzalishaji na uuzaji wa nishati ulimwenguni.

Watendaji hao wakiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji  wa TotalEnergies Tanzania, Jean Francois Schoepp walifika Wizara ya Nishati kutambulisha rasmi mabadiliko yaliyofanyika ndani ya kampuni hiyo ambapo kwa sasa badala ya kujikita kwenye mafuta na gesi pekee, wameanza kujishughulisha na masuala ya nishati jadidifu pia.

Kampuni hiyo ilimweleza Waziri wa Nishati nia ya kuwekeza Tanzania kwenye miradi ya kuzalisha umeme kwa kutumia nishati jadidifu kama vile Jua na Upepo kutokana na uhakika wa upatikanaji wa vyanzo hivyo vya nishati ya umeme.

Waziri wa Nishati ameieleza kampuni kuwa nia ya Serikali ni kuwa na umeme wa uhakika unaotokana na vyanzo mbalimbali ikiwemo Nishati Jadidifu hivyo kinachotakiwa ni kufanya taratibu zitakazowawezesha kufanya uwekezaji huo.