Hafsa Omar-Dar Es Saalam

Waziri wa Nishati, January Makamba amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Uganda nchini Tanzania, Balozi  Richard Kabonero.

Mazungumzo hayo, yamefanyika Novemba 15, 2021 katika ofisi ndogo za Wizara ya Nishati zilizopo jijini Dar es Saalam.

Katika kikao hicho ambacho walijadili maandalizi ya ziara ya Rais wa Uganda, Yoweri Museveni ambae anatarajiwa kuanza ziara nchini Tanzania hivi karibuni.

Aidha, Makamba alisema kuwa Uhusiano mzuri uliopo baina hizo nchi hizi mbili  umepelekea kurahisisha ujenzi wa Bomba la kusafirisha mafuta ghafi la Afrika Mashariki ( EACOP) na Marais wa nchi  hizo mbili watahakikisha kuwa mradi huo unakamilika.

Pia, alisema mradi wa EACOP ni muhimu sana katika nchi hizo mbili  na mpaka sasa upo kwenye hatua nzuri.

“Tunafurahi hatua kubwa iliyofikiwa katika mradi na tunajua umuhimu wa mradi huu kwa nchi zetu zote mbili,” alisisitiza Waziri Makamba.

Kwa upande wake, Balozi wa Uganda nchini Tanzania, Balozi Richard Kabonero ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano waliotoa kwa kuhakikisha mradi wa Bomba la mafuta unafanikiwa.