Na Munir Shemweta, KAGERA
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula amewataka wamiliki wa ardhi nchini kuhuisha milki zao zilizoisha muda wake ili kuepuka kufutiwa ardhi wanayomiliki kwa mujibu wa sheria.

Sheria ya Ardhi Na 4 ya mwaka 1999 inamtaka mmiliki wa ardhi kuhuisha miliki yake baada ya muda wa awali aliopewa kuisha. Mmiliki huyo anatakiwa kuomba kuongezewa muda wa kumiliki ardhi na mamlaka husika inawajibu wa kumuongezea ama kutomuongezea kulingana na masharti ya umiliki ambayo ni pamoja na kufanya maendelezo katika eneo analomiliki.

Akizungumza na watendaji wa sekta ya ardhi pamoja wananchi waliowakabidhi hati za ardhi tarehe 22 Novemba 2021 kwenye ukumbi wa Manispaa ya Bukoba, Naibu Waziri Mabula alisema, watendaji wa sekta ya ardhi wanatakiwa kuangalia namna ya bora ya kuwafikia wale wote ambao hati zao za umiliki ardhi zimeisha muda wake.

Akitolea mfano wa Manispaa ya Bukoba Dkt Mabula alisema, kuna milki takriban 22 katika manispaa hiyo zimeisha muda na wamiliki wake bado hawajajitokeza kuhuisha na kuwataka watendaji wa sekta ya ardhi kwenda eneo hilo kuwakumbusha ili waweze kuhuisha milki zao.

Aidha , Naibu Waziri wa Ardhi Dkt Mabula aliwataka watendaji wa sekta ya ardhi kuhakikisha wanatoa elimu kwa wamiliki wa ardhi kuhusiana na umuhimu wa kuhuisha milki zao  zilizokwisha muda na kufafanua kuwa kutofanya hivyo kutasababisha mmiliki hizo kufutwa.

" Kama umepewa hati ya miaka 33 au 69 halafu muda wake umeimeisha na wengi wenye hati za aina hiyo muda wake 'umeexpire' unatakiwa kuihuisha hati na wasipofanya hivyo ardhi unayomiliki anaweza kupatiwa mmiliki mwingine na hatua hiyo inaweza kuleta manung'uniko wakati uamuzi umefanyika kisheria" alisema Dkt Mabula.

Hata hivyo, Naibu Waziri Mabula amewataka watendaji wa sekta ya ardhi kutotumia fursa ya kuisha muda wa umiliki kuwanyang'anya wamiliki maeneo yao na badala yake wahakikishe wanatoa elimu ya kuhuisha sambamba na kufuata sheria wakati wa kutekeleza sheria.

Baadhi ya wananchi wa Manispaa ya Bukoba mkoani Kagera wametaka kuwepo utaratibu wa kuwakumbusha wamiliki ardhi kuhuisha hati zao pale muda wake unapokuwa umeisha ili kuepuka milki hizo kufutwa bila wao kujua.

Diwani wa Kata ya Katerero mkoani Kagera Bw Nuru Kabendera mbali na kushukuru ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Kagera kuwapatia Hati katika kipindi kifupi lakini amesema wengi wa wamiliki bado hawajui muda wa kuisha kwa hati na kutaka elimu ya uhuishaji kutolewa hadi yale maeneo ya vijijni ili wamiliki waweze kufahamu.

Naye mkazi wa kata ya Bakoba mtaa wa Nyakanyasi Manispaa ya Bukoba Bi. Grace Kokuledi amewaasa wamiliki wa ardhi kuwashirikisha watoto wao katika suala zima la umiliki ardhi ili iwe rahisi kwao kuhuisha miliki pale itakapotokea Mungu amewachukua kwa kuwa hati hizo umiliki wake unafikia hadi miaka 99.