WAZIRI wa Afya, Maendeeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima amesema, Tanzania inatumia chanjo kama nyenzo ya kujikinga katika kudhibiti madhara ya janga la UVIKO-19 kupitia mpango wa dunia wa COVAX ambapo Tanzania imeetengewa chanjo 12,049,827 na tayari imepokea chanjo 1,223,400 ya aina ya Janssen, 1,065,600 za Sinpharm na chanjo 500,000 za Pfizer ambazo zinaendelea kutolewa katika maeneo mbalimbali nchini.

Waziri Gwajima ameeleza hayo wakati akifungua mkutano wa 22 wa mapitio ya pamoja ya Sera ya mwaka ya sekta ya Afya jijini Dar es Salaam kwa kauli mbiu ya ''Ustahimilivu wa Mfumo ya Afya katika Mapambano Dhidi ya UVIKO-19, Kujenga Mfumo Thabiti Kupitia Uzoefu wa Kukabiliana na Janga Hilo'' Waziri Gwajima amesema zoezi la utoaji chanjo linaendelea ili kufikia malengo ya kuwafikia wananchi kwa asilimia 60 na hiyo ni pamoja na kutekeleza mapendekezo 19 ambayo yalifanyiwa kazi na kamati ya ushauri ya Rais.

Waziri Gwajima amesema mkutano huo ni maalum kwa kujadili sera, mwelekeo wa sekta ya afya katika kuangalia taarifa ya viashiria muhimu katika sekta hiyo pamoja na utekelezaji wake pamoja na.

Amesema Sekta ya Afya amekuwa na mafanikio mengi kwa mwaka 2021/2022 ikiwemo ongezeko la wanawake wajawazito wanaohudhuria kliniki mara nne zaidi katika mahudhurio yao pamoja na asilimia 83 za wanawake na watoto wanaohudhuria kliniki ujenzi wa vituo vya afya katika kila Wilaya huku akieleza changamoto kubwa ikiwa ni upungufu wa watumishi.

Waziri Gwajima amewashauri wadau kushirikiana na Serikali katika kutoa elimu kwa umma kuhusiana na bima ya afya ambao hadi sasa ni asilimia 14 pekee huchangia mfuko huo kwa utaratibu na mfumo wa ulazima uliowekwa.

Pia Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Dkt. Festo Dugange amesema sekta ya afya imekuwa ikiendelea kuimarika na hadi kufikia Novemba 21 Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan ilitoa Bilioni 55.25 kwa kuimarisha sekta ya afya kwa maeneo 221 ya kimkakati.

Amesema mapendekezo ya kuimarisha sekta hiyo zaidi ni kuhakikisha matumizi ya TEHAMA katika vituo vya afya pamoja na viongozi wa ngazi za halmashauri na Wilaya kuhamasisha jamii juu ya umuhimu wa bima ya afya.

Amesema, Serikali imenunua vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi bilioni 95.37 kupitia mkopo nafuu wa mfuko wa IMF na vifaa hivyo vimepelekwa kwenye vituo vya afya nchini.

Kwa upande wake Mkurugenzi mkazi wa USAID Kate Somvongsiri amesema nchi nyingi duniani ikiwemo Tanzania zimeathirika na mlipuko wa virusi vya Corona na Serikali ya Tanzania imekuwa mstari wa mbele kwa kuchukua tahadhari ikiwemo kutoa chanjo ili kukabiliana na maambukizo ya virusi hivyo.

Amesema ni muhimu serikali kuangalia utekelezaji wake kwa kushirikiana na sekta binafsi na za afya na wao wataendelea kushirikiana na Serikali katika kuboresha huduma za afya na miundombinu yake ikiwemo dawa na vitendanishi.

Amesema tahadhari zinazoendeelea kuchukuliwa dhidi ya UVIKO-19 pia ziendelee kuchukuliwa kwa magonjwa mengine yanayoambukiza ikiwemo UKIMWI ili kuboresha afya ya ustawi jamii kwa kuwa Afya ni kipaumbele zaidi.

Mkutano huo umehudhuriwa na viongozi wa Serikali, wadau wa maendele katika sekta ya afya, sekta binafsi, taasis za tafiti na mashirika yasiyo ya kiserikali.