Na. WAMJW

Rais wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan amewatunuku Cheti na Nishani Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dorothy Gwajima na Katibu Mkuu Wizara ya Afya Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii Dkt John Jingu kwa utumishi uliotukuka na kuchambua mchango wao katika utekelezaji wa majukumu yao.

 

Akipokea Cheti na Nishani hiyo aliyokabidhiwa kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mlezi wa Chama cha Skauti. Bi Mwantumu B. Mahiza jijini Dar Es Salaam Waziri Dkt Gwajima amemshukuru Rais Samia Suluhu kwa kutambua mchango wake katika kuwatumikia wananchi akiwa ni Waziri wa Sekta ya Afya na Maendeleo ya Jamii.

 

Taasisi ya Skauti Tanzania hutoa cheti na nishani ya "Medal of Gold" kwa Viongozi mbalimbali kutambua mchango wao katika kutekeleza majukumu yao.

 

Aidha Dkt. Gwajima amewashukuru watumishi na wadau wote wa Sekta ya Afya na Maendeleo ya Jamii na kusema kuwa cheti na nishani hiyo ni heshima kwa Wadau wote wa Sekta ya Afya na itachochea zaidi Ari na Kasi ya kazi katika kushirikiana na Skauti Tanzania.

 

"Hii nishani siwezi kusema ni yangu bali ni yangu na wenzangu wote katika Wizara ninayoitumikia. Niwashukuru sana watumishi na wadau wanaofanya kazi na Wizara katika kutekeleza majukumu yetu ya kuihudumia jamii", amesema Mhe. Gwajima.

 

Katika hatua nyingine Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto (Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii) Dkt. John Jingu naye pia ametunukiwa nishani ya utumishi uliotukuka katika kupambana na ukatili dhidi ya watoto kutoka kwa Taasisi ya Skauti Tanzania.