MENO  mawili ya Tembo  yamekamatwa na Kikosi maalum Cha kupambana na ujangili katika eneo la Jumuiya ya  hifadhi ya Wanyamapori  Burunge, wilayani Babati mkoa wa Manyara baada ya kufanya upekuzi katika Nyumba ya mtuhumiwa wa ujangili.

Kamanda wa Kikosi cha kuzuia ujangili (KDU) Kanda ya Kaskazini,Peter Mbanjoko amesema meno hayo yamekamatwa Kijiji cha Kakoi wilayani Babati mkoa wa Manyara.

Amesema kikosi cha kupambana na ujangili ambacho kinahusisha askari wa Taasisi ya Wanyamapori (TAWA) askari wa hifadhi ya Tarangire, askari ya Burunge WMA na askari wa Taasisi ya chemchem iliyowekeza katika eneo Hilo ndio wamefanikisha kukamatwa Meno hayo yakiwa yamefichwa ndani.

Mbanjoko  amesema hata hivyo  mtuhumiwa alikimbia Kabla ya kutiwa mbaroni na bado anasakwa lakini anashikiliwa mkewe Kwa mahojiano zaidi na yupo kituo kikuu Cha Polisi Babati Mkoani Manyara.

"Naomba nitoe onyo Kwa majangili waache kuendelea na ujangili wajue lazima watakamatwa,"amesema.

Meneja wa taasisi ya chemchem,Walter Pallangyo amesema kuendelea kukamatwa Kwa watuhumiwa kunatokana na kuimarishwa  operesheni ambapo Taasisi Yao ambayo imewekeza hoteli za kitalii imetenga kutumia shillingi milioni 400 Kila mwaka kupambana na ujangili.

Hata hivyo pallangyo alisema kuendelea kuongezeka shughuli za kibinaadamu katika maeneo ya hifadhi na mapito ya wanyama imekuwa chanjo Cha kuendelea ujangili.

Amesema uvamizi mkubwa maeneo ya hifadhi na mapito ya wanyama unaoendelea nawananaomba Wizara ya Maliasili na Utalii kukamilisha mchakato wa kuweka mipaka lakini pia kutengwa maeneo ya hifadhi na shughuli Nyingine.

Ameongeza Taasisi Yao Kwa kushirikiana na Burunge WMA , halmashauri ya Babati na Mkoa tayari waliandaa vikao kadhaa kutaka kulindwa maeneo ya hifadhi na mapito.

"Tunaomba Wizara ya Maliasili kukamilisha taratibu za kulinda eneo la mapito ya wanyama ambalo lipo Kati Kati ya hifadhi ya Taifa ya Tarangire na Manyara ili kuendeleza Uhifadhi,"amesema.