Serikali ya Marekani imetangaza dau la hadi dola milioni 5 kwa yeyote mwenye taarifa zitakazowezesha kukamatwa au kutiwa hatiani kwa raia wanne wa Mexico wanaotuhumiwa kwa ulanguzi wa dawa za kulevya. 

Miongoni mwa hao wanne ni Aureliano Guzman-Loera ambaye ni kaka wa Joaquin "El Chapo" aliyetiwa hatiani na kufungwa jela mwaka 2019 kwa kuingiza mamilioni ya kilogramu za dawa za kulevya nchini Marekani chini ya genge la uhalifu liitwalo Sinaloa. 

Wizara ya sheria ya Marekani imesema pia inatafuta taarifa za ndugu watatu wa familia ya Nevarez ambao wanafanya kazi chini ya mwavuli wa kundi la Sinaloa linaloendesha mtandao mkubwa wa usafirishaji dawa za kulevya duniani. 

Miongoni mwa makosa yanayowakabili ni kuingiza dawa aina ya fentanyl ambayo kati ya mwaka 2020 hadi 2021 inahusishwa na asilimia 63 ya vifo vya matumizi yaliyopindukia ya dawa za kulevya nchini Marekani.