Kesi ya ugaidi inayomkabili mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na wenzake watatu imeahirishwa hadi kesho kutokana na kutokukamilika kuandikwa uamuzi kuhusu uhalali wa shahidi wa Jamhuri anayedaiwa kupanda kizimbana akiwa na diary, simu na kalamu

Akitoa uamuzi huo leo Jumanne Novemba 16, 2021 Jaji Joachim Tiganga amesema ameshindwa kukamilisha kuandika uamuzi huo kutokana na wingi wa hoja zilizotolewa na mawakili wa pande zote.

Jana yaliibuka malumbano ya kisheria katika mahakama hiyo kuhusiana na uhalali wa shahidi kupanda kizimbani akiwa na diary, simu na kalamu.

Upande wa utetezi unadai kuwa shahidi huyo alikuwa anatumia vifaa hivyo wakati akitoa ushahidi wake Ijumaa, jambo wanalosisitiza kuwa ni kinyume cha sheria na utaratibu.