Na. Peter Haule na Josephine Majura, WFM, Dar es Salaam
Kamishna wa Maendeleo ya Sekta ya Fedha nchini, Dkt. Charles Mwamwaja amesema kuwa watanzania chini ya asilimia 50 ndio waliofikiwa na huduma za fedha jambo ambalo limeifanya Serikali kuwa na Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa ili kuongeza uelewa kwa wananchi kwa lengo la kuchochea ustawi wa jamii.

Hayo ameyabainisha wakati akitembelea mabanda katika maonesho ya Wiki ya Fedha yanayoendelea katika viwanja vya Mnazi Mmoja Jijini Dar es Salaam ikiwa ni siku ya kwanza ya maonesho hayo.

Alisema huduma za fedha zinarahisisha utaratibu wa kubadilishana bidhaa na huduma jambo ambalo ni muhimu katika maendeleo ya uchumi kwa nchi yeyote Duniani ikiwemo Tanzania hivyo ni lazima kuwa na mkakati wa kutoa elimu kwa umma kuhusu uelewa wa huduma hiyo.

“Watu wanadhulumiwa na hawajui waende wapi, nani ni mtoaji wa huduma hiyo rasmi, mteja akidhulumiwa aende wapi  na hawajui kuwa mteja wa huduma za fedha analindwa, hivyo Serikali imeamua kutoa elimu kwa umma ili kuondoa sintofahamu hiyo”. alieleza Dkt. Mwamwaja

Dkt. Mwamwaja alisema kuwa Sekta ya Fedha inarahisisha upatikanaji wa mitaji na uwekezaji ndio maana vikundi vidogo vya kuweka na kukopa kama Vikoba, vinasaidia kukuza mitaji ambayo inaweza kutumika kuwekeza kwenye miradi ya ufugaji na mingine ambayo inamanufaa si tu kwa mtu mmoja mmoja bali kwa Taifa kwa ujumla.

Aidha alisema matokeo chanya ya Sekta ya Fedha hayawezi kufikiwa bila kuwekeza katika elimu ili wananchi waweze kutumia fursa zilizopo kwa maendeleo yao na nchi kwa ujumla.

Vilevile Dkt. Mwamwaja alisema umbo la Sekta ya Fedha limegawanyika katika maeneo matano  ambayo ni masuala yanayohusiana na huduma za Benki, Bima, Masoko ya Mitaji na Dhamana, Mifuko ya Jamii na Huduma ndogo ya Fedha.

Maonesho ya Huduma za Fedha Kitaifa yameanza Novemba 8 na kutarajiwa kuhitimishwa Novemba 14 mwaka huu katika Viwanja vya Mnazi Mmoja, jijini Dar es Salaam.