Polisi mkoani Songwe wanawashikilia watu 24 wa Kijiji cha Chang'ombe wilayani Songwe kwa tuhuma za kuzingira kituo cha polisi Galula.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Songwe, Janeth Magomi amesema watu hao walivamia kituo wakishinikiza kurejeshewa mikoba ya waganga wa jadi (lambalamba) iliyokamatwa na askari wa kituo hicho.

Amesema watu hao walikizingira kituo hicho Novemba 22, 2021 alfajiri baada ya askari kuzuia kazi za lambalamba wanaowadhalilisha watu wakiwatuhumu ni wachawi.

Amesema kufuatia tukio hilo Mwenyekiti wa Kijiji na watu wengine 23 wanashikiriwa polisi kwa ajili ya uchunguzi zaidi.

Hivi karibuni Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Omary Mgumba akiwa Mji Mdogo wa Mlowo aliwataka wakazi wa mkoa huo kuachana na wapiga ramli chonganishi wakiwamo lambalamba.