Umoja wa Afrika umetangaza  kwamba umesimamisha uanachama wa Sudan katika Umoja huo wa mataifa wanachama 55 baada ya mapinduzi ya kijeshi kuiondoa madarakani serikali ya mpito siku ya Jumatatu. 

Kulingana na taarifa ya baraza la usalama na amani la Umoja huo, hatua hiyo inaanza kutekelezwa mara moja na kuizuia Sudan kufanya shughuli zozote za Umoja wa Afrika hadi kurejeshwa madarakani kwa serikali ya mpito inayoongozwa na raia. 

Baraza hilo la amani na usalama pia limemtaka mwenyekiti wa Umoja huo kumtuma mjumbe nchini Sudan ili kuwasiliana na wadau nchini humo kuhusu hatua zinazohitajika ili kuharakisha kurejesha utaratibu wa kikatiba nchini humo.