Na. WAMJW – Kilimanjaro
Waziri wa Afya,Maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto Dkt Dorothy Gwajima amesema Tanzania ni miongoni mwa nchi 70 ulimwenguni zinazofanya Utafiti wa Afya ya Uzazi na Mtoto ambapo kwa mara ya kwanza utafiti huu ulifanyika mwaka 1991-92 na umeendelea kufanyika takribani kila baada ya miaka mitano na utafiti wa mwaka 2021-22 utakuwa ni utafiti wa sita kufanyika.

Dkt. Gwajima amebainisha hayo jan wakati wauzinduzi wa mafunzo kwa washiriki wa Utafiti wa Afya ya Uzazi na Mtoto na viashiria vya Malaria Tanzania wa Mwaka 2021-22 (2021-22 Tanzania Demographic and Health Survey and Malaria Indicator Survey) Mkoani Kilimanjaro.

Dkt, Gwajima amesema
Kwa mujibu wa takwimu rasmi kutoka katika Ofisi ya Taifa ya Takwimu katika robo ya pili ya mwaka 2021 yaani Aprili hadi Juni 2021 sekta ya Afya imeendelea kukua kwa asilimia 4.8 na Pato la Taifa kwa kipindi hicho limekua (growth) kwa asilimia 4.3 hii ikiwa ni ishara inayoonesha kuwa afya za wananchi zinaimarika.

Kwa sasa Mwenendo wa vifo vitokanavyo na uzazi vimekuwa vikipungua duniani ambapo vimepungua kwa asilimia 38 kutoka vifo 342 mwaka 2000 hadi 211 mwaka 2017 kwa kila vizazi hali 100,000 kwa makadirio ya Kanzidata ya Umoja wa Taifa (UN- DataBase for Data Flows)

Kwa upande wa Bara la Afrika na hususan kwa nchi zilizo Kusini mwa Jangwa la Sahara, vifo vinavyotokana na uzazi vilipungua kutoka wanawake 870 mwaka 2000 hadi wanawake 533 mwaka 2017 kwa kila vizazi hai 100,000.
Vilevile, kwa Tanzania, vifo hivi vilipungua kutoka vifo 910 mwaka 1990/91 hadi 432 kwa kila vizazi hai 100,000 mwaka 2012 kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012 ambayo ilihoji wanawake wote nchini wenye umri wa miaka 15 hadi 49.

“Katika Mpango wa Tatu wa Taifa wa Maendeleo tulijiwekea malengo ya kupunguza vifo hivi kutoka vifo 220 mwaka 2020/21 hadi 180 mwaka 2025/26”, amesema Waziri Gwajima

Aidha Dkt Gwajima ameendelea kusema kuwa vifo vya watoto wachanga Tanzania vimepungua kutoka vifo 92 kwa kila watoto wanaozaliwa hai 1,000 mwaka 1991/92 hadi vifo 43 kwa watoto wanaozaliwa hai 1,000 mwaka 2015/16.

Dkt,Gwajima ameeleza kuwa serikali imekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha Wanawake na Watoto wanapewa huduma bora za afya akiitolea mfano kampeni ya ‘Jiongeze Tuwavushe Salama’, ambayo lengo lake ni kuhakikisha akina mama wajawazito na watoto wanapata huduma bora.

Dkt.Gwajima amesema kuwa muasisi wa kampeni hiyo ni Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ambaye alianzisha kampeni hiyo kipindi alipokuwa Makamu wa Rais.

Kauli Mbiu ya Utafiti wa Afya ya Uzazi na Mtoto na Malaria wa mwaka 2021-22 ni “Leave No One Behind” – “Hakuna atakayeachwa Nyuma”.

Sambamba na hayo Dkt, Gwajima ametoa wito kwa Wananchi wote kuitikia wito wa Serikali wa Kuchanja Chanjo ya UVIKO-19, ambapo chanjo hiyo inatolewa kwa hiari.