Na Steven Nyamiti-WM
WAZIRI wa Madini, Dkt. Doto Biteko ameagiza Leseni za uchimbaji wa madini zisizoendelezwa zifutwe ili maeneo hayo wapewe wachimbaji wenye nia ya kuchimba madini.

Dkt. Biteko ametoa maagizo hayo  jana Oktoba 7, 2021 kwenye ziara yake ya kikazi wilayani Kyerwa Mkoa wa Kagera wakati akizungumza na wachimbaji na wafanyabiashara wa madini ya Bati ambapo pia ametembelea Soko Kuu la madini hayo.
 

Aidha, ameagiza kuwa kufikia Novemba 25, 2021 Tume ya Madini isitishe utaratibu wa utozaji wa mrabaha wa madini ujenzi kwa kutumia vitabu vya risiti badala yake ufanyike kwa taratibu za kiserikali kupitiaMashine za Risiti za Kielektroniki (POS).

“Tutoke kwenye utozaji wa mrabaha wa madini ujenzi kwa kutumia Stakabadhi za Kitabu kwenda kwenye Mfumo wa Risiti za ‘Electronics’ (Mashine za Risiti za Kielektroniki (POS),”amesema.
 

Naye, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Kagera,Mhandisi Lucas Mlekwa, amesema Ofisi ya Madini Mkoa wa Kagera unaendelea kutoa hati za makosa ( Default Notice) na kuzifuta leseni ambazo haziendelenzwi na wamiliki.

Akizungumzia makusanyo ya maduhuli ya Serikali, Injinia Mlekwa ameeleza kuwa, ukusanyaji wa maduhuli katika Mkoa wa Kagera umeendelea kuongezeka kutokana na marekebisho ya Kanuni ya Uongezaji thamani hivi karibuni.

“Katika Mwaka wa Fedha 2021/2022 ofisi ya madini Kagera imepangiwa kukusanya kiasi cha Fedha 4.57 Bilioni na ndani ya miezi mitatu Julai hadi Septemba 2021 jumla ya shilingi 1,060,0356,767.02 zimekusanywa sawa na asilimia 92.81 ya lengo la makusanyo kwa miezi mitatu,” amesema Mlekwa.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kyerwa, Rashidi Mwaimu, amempongeza, Dkt. Biteko kwa kazi nzuri anayoifanya ya kusimamia Sekta ya Madini ambapo amewataka wachimbaji wa madini ya Bati kuwa wazalendo kusimamia rasilimali za nchi.

Mkoa wa Kagera umejaliwa kuwa na madini ya aina mbalimbali katika wilaya zake ikiwemo madini ya ujenzi na madini ya viwanda, dhahabu na Bati.