Na Munir Shemweta, WANMM DODOMA
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula amefanya ziara ya kushtukiza ofisi ya ardhi ya halmashauri ya jiji la Dodoma na kuagiza maombi 521 ya umilikishaji ardhi katika ofisi hiyo kukamilishwa ndani ya siku tatu.

Akiwa ameambatana na Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Mary Makondo na Menejimenti ya Wizara katika ziara hiyo tarehe 25 Oktoba 2021 jiji Dodoma, Dkt Mabula alisema, pamoja na kuwepo changamoto lakini anachohitaji maombi 521 yawe yamekamilika katika kipindi cha siku tatu.

‘’Kuanzia sasa tunahitaji zile ‘application’ zote ambazo hati zake watu wameomba zitoke ndani ya siku tatu kama ni kutoka saa nane za usiku tunahitaji hiyo kazi ikamilike ndani ya siku tatu’’ alisema Dkt Mabula.

Aidha,aliwataka watendaji  wa sekta ya ardhi katika jiji la Dodoma kuandaa hati zisizopungua mia moja  kwa siku moja sambamba na kuwataka kumhakikishia kwa maandishi ahadi walizompa katika kutekeleza maagizo yake.

Uamuzi wa Naibu Waziri wa Ardhi kufanya ziara ya kushtukiza ofisi ya ardhi katika jiji la Dodoma unafuatia kujitokeza baadhi ya malalamiko ucheleweshaji umilikishaji ardhi kwa wananchi wa mkoa wa Dodoma jambo lililofanya wizara kuanza mkakati maalum wa ukwamuaji na uharakishaji utoaji hati kwenye jiji hilo.

Awali Naibu Waziri Dkt Mabula na timu yake walitembelea vitengo vya ardhi katika halmashauri ya Jiji la Dodoma ili kubaini baadhi ya changamoto katika sekta hiyo.

Dkt Mabula alisema, jiji la Dodoma ndiyo sura ya nchi hivyo Maafisa wake wa ardhi wanatakiwa kuwapanga wananchi wanaokwenda kupata huduma kulingana na maeneo wanayotoka sambamba na maafisa hao kuvaa vitambulisho ili kutambulika kwa wananchi.

‘’Hatuihitaji kusikia kelele za watu hapa, ninyi mnachafua image ya Wizara na sekta kwa sababu tu ya kutojipanga kwenye utendaji wenu wa kazi, mko wengi mnaweza kujipanga vizuri pamoja na kuwepo upungufu wa watumishi kwa baadhi ya maeneo’’ alisema Dkt Mabula.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mary Makondo alieleza kuwa, wizara yake imejipanga kuhakikisha inaongeza kasi ya umilikishaji ardhi katika mkoa wa Dodoma na Maeneo mengine nchini.

Katika jitihada za ukwamuaji na kuongeza kasi ya utoaji hati katika jiji la Dodoma, Wizara yake imeamua kuongeza nguvu ya watumishi kutoka Makao Makuu ili kuharakisha kasi ya utoaji hati kwa wamiliki wa ardhi.

Kaimu Mkuu wa Idara ya Ardhi na Mipango Miji Halmashauri ya jiji la Dodoma Amelyo Chaula aliweka wazi kuwa, mwamko mkubwa umilikishaji ardhi kutoka kwa wananchi umesababisha ofisi yake kuelemewa na kazi. Hata hivyo, alisema ofisi hiyo imekuwa ikifanya juhudi kubwa kuhakikisha wananchi wanapatiwa huduma kwa wakati pamoja na kuwepo changamoto kadhaa kwa baadhi ya maeneo hasa yale yaliyorithiwa kutoka iliyokuwa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA na kusisitiza kuwa maeneo mapya hayana changamoto ya Umilikishaji.