Mwandishi wa vitabu vya  riwaya na hadithi fupi fupi  kutoka nchini Tanzania Abdulrazak Gurnah  ndio mshindi wa mwaka huu wa tuzo ya Nobel ya Fasihi.

Kamati inayotoa tuzo hiyo imemtangaza Gurnah kuwa mshindi wa tuzo hiyo kufuatia kazi yake ya uandishi kuhusu athari za ukoloni na hatima ya wakimbizi katika eneo la ghuba, baina ya tamaduni na mabara.

Mzaliwa wa Visiwani Zanzibar aliwasili Uingreza kama mkimbizi katika miaka ya mwisho ya 1960 na kuwa Profesa katika Chuo Kikuu cha Kent, amechapisha riwaya 10 na hadithi fupi fupi kadhaa.

Hata hivyo, kazi yake iliyomtambua, ni riwaya aliyoandika mwaka 1994 na kuipa jina Paradise, kuelezea hali ya ukoloni katika eneo la Afrika Mashariki wakati wa vita vya kwanza vya dunia.

Akimtangaza mshindi wa tuzo hiyo ya nobel kuhusu fasihi, Mwenyekiti wa Kamati ya Nobel Anders Olsson, amemtaja Gurnah mwenye umri wa miaka 73, kama Mwandishi mahiri baada ya nchi za Afrika kupata uhuru.

Tangu tuzo ya kwanza kutolewa mwaka 1901, kwa asilimia 80, waliopata tuzo hii ya Fasihi, wamekuwa ni Wazungu wanaotokea barani Ulaya na America Kaskazini.

Tuzo hii inakuja na Dola Milioni 1.4 na Gurnah atakabidhiwa fedha hizo kutoka kwa Kamati hiyo ya Nobel kutoka nchini Sweden.