Na Dotto Mwaibale
MKURUGENZI Mkuu wa Bohari ya Dawa  (MSD) Meja Jenerali Gabriel Saul Mhidze amesema MSD inaendelea na mpango wa usambazaji dawa, vifaa tiba na vitendanishi vya maabara kama moja ya jukumu lake kwa kasi kubwa ambapo hadi kufikia Oktoba 16 hakutakuwa na kituo cha kutolea huduma za afya nchini chenye uhaba wa bidhaa za afya.
 

Amesema agizo la Waziri Mkuu la kuitaka MSD kupeleka dawa vituoni ndani ya siku saba limekuja na msukumo mkubwa kwani MSD kwa sasa imeongeza masaa zaidi ya kufanya kazi hususani kwenye maghala ya kupokelea dawa.
 

Ameongeza kuwa MSD husambaza dawa kwa kuzingatia mzunguko (ILS),yaani mara nne hadi sita kwa mwaka, lakini kutokana na agizo la Waziri Mkuu, wamechukua hatua ya kupeleka dawa hizo pindi zinapopokelewa nia ni  kuhakikisha vituo vyote vyenye uhitaji vinapokea dawa.
 

Meja Jenerali Mhidze, amesema mpaka sasa MSD imepokea makontena 16 ya dawa zenye thamani ya takribani bilioni 43 huku nyingine zikiwa njiani.
 

Alisema mbali na usambazaji huo, shehena nyingine za dawa Tani 12 zitawasili nchini alhamisi kupitia uwanja wa ndege, huku Oktoba 16 shehena yenye Tani 12 ikitarajiwa kuingia na makontena 18 yenye dawa yanatarajiwa  kuwasili nchini wakati wowote kuanzia kesho kutwa.
 

Meja Jenerali Mhidze, alisema dawa hizo zipo zitakazowasili nchini kwa kutumia ndege na bahari, lengo likiwa ni kumaliza tatizo la uhaba wa dawa lililojitokeza.