Issa Mzee    -Maelezo
Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Christopher Kadio, amesema Rasimu ya Sera ya Kinga ya Usafirishaji Haramu wa Binadamu na Kinga ya Uhamaji haramu katika Bara la Afrika, inatarajiwa kufikishwa kwa Mawaziri husika ili kuthibitishwa rasmi kwa lengo la kupiga vita biashara haramu Afrika.

Hatua hiyo imefikiwa baada ya sera hizo kujadiliwa kwa kina na timu ya kiufundi kutoka mataifa 55 wa Umoja wa Afrika (AU), katika kikao maalumu kilichoandaliwa na Tume ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Afrika(AUC), kilichofanyika kwa muda wa siku tatu katika hotel ya Madinat Al Bahri, Mbweni Mjini Zanzibar.

Kadio alisema majadiliano ya sera hizo yameifikiwa katika hatua nzuri ambayo yatasaidia kuengeza nguvu ya kupambana na uhalifu huo unaopelekea uvunjifu wa haki za binadamu kwa waafrika.

Alieleza kuwa, Tanzania ni miongoni mwa nchi zinazopiga vita usafirishaji haramu wa binadamu, hivyo kufanyika kwa majadiliano hayo yataziwezesha nchi za Afrika ikiwemo Tanzania kuwalinda raia wake na kuaweka salama.

Nae Katibu Sekretarieti ya Kitaifa ya Kuzuwia na Kupambana na Biashara Haramu ya Usafirishaji wa Binadamu, Seperatu Fela, alisema mkutano huu umewawezesha wajumbe kuzipitia sera na utasaidia kuwaunganisha waafrika ili kupata nguvu ya pamoja ya kupiga vita uhalifu huo.

Alieleza kuwa, jitihada zinazoendelea kufanywa na wanajumuiya wa Umoja wa Afrika zitasaidia kwa kiasi kikubwa katika kupiga vita usafirishaji wa binadamu kwa njia ya haramu pamoja na uhamaji haramu.

Miongoni mwa sababu zinazopelekea waafrika kufanyiwa uhalifu huo ni umasikini, ukosefu wa ajira pamoja na machafuko ya kisiasa.

Miongoni mwa mapendekezo yaliyotolewa katika mkutano huo ni kufanyika kwa mazungumzo baina ya wanaharakati wa Afrika wanaopiga vita uhalifu huo na Mataifa yanayoshiriki katika uhalifu huo nje ya Afrika.