Mikoa ya Lindi, Mara na Dodoma, imetajwa kinara kwa kuwa na kiwango kikubwa cha ufaulu wa mtihani wa darasa la saba, katika kipindi cha miaka mitatu mfululizo.

Taarifa hiyo imetolewa jana  Jumamosi, tarehe 30 Otoba 2021 na Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA), Dk. Charles Msonde, akitangaza matokeo ya mitihani hiyo ya kumaliza elimu ya msingi, jijini Dar es Salaam.

Dk. Msonde amesema, mkoa wa kwanza ulioongoza ni Lindi, ukifuatiwa na Mara huku wa tatu ukiwa ni Dodoma.

“Ukiangalia halmashauri kwa miaka mitatu mfululizo, zimekuwa zikiongeza ufaulu na hazijawahi kushuka, ya kwaza ni Liwale mkoani Lindi, Uvinza (Kigoma), Butiama (Mara), Mtama (Lindi), Musoma (Mara), Chemba (Dodoma), Kasulu TC (Kigoma), Hanang, Bahi na Kondoa Mji (Dodoma),” amesema Dk. Msonde.

Aidha, Dk. Msonde ameitaja mikoa 10 iliyofanya vizuri kwa ufaulu wa mtihani huo, ambapo wa kwanza ni Dar es Salaam, ukifuatiwa na mikoa ya Iringa, Mbeya, Arusha, Njombe, Kilimanjaro, Katavi, Lindi, Simiyu na Pwani.

Kwa upande wa halmashauri zilizofanya vizuri ni, Halmashauri ya Ilala, Arusha, Kinondoni, Moshi Manispaa, Mwanza Manispaa, Iringa Manispaa, Ilemela, Mafinga Mji na Kigamboni Manispaa.