Watu wawili wamefariki dunia na wengine zaidi ya 30 wamelazwa hospitalini, baada ya kula nyama ya ng’ombe anayesadikiwa kuwa na ugonjwa wa kimeta wilayani Rombo mkoani Kilimanjaro.

  Mkuu wa mkoa Kilimanjaro, Stephen Kagaigai amesema watu hao walikula nyama hiyo baada ya mtu aliyejifanya mtaalamu wa mifugo kuthibitisha nyama hiyo ni salama na kuipiga mihuri bandia.

  Amesema kufuatia tukio hilo, Jeshi la polisi mkoani Kilimanjaro linamshikilia mtu huyo anayedaiwa kujifanya mtaalamu ambaye anaendelea kupatiwa matibabu katika hospitali ya Ngoyoni wilayani Rombo huku hali yake ikielezwa kuwa ni mbaya.

  Mkuu huyo wa mkoa wa Kilimanjaro amefafanua kuwa, katika eneo la Mamsera nyumbani kwa mwananchi mmoja kulikuwa na ng’ombe watatu na mmoja alikufa, baadaye alijitokeza mtu huyo na kudai kuwa ni mtaalamu wa mifugo akathibitisha ng’ombe yule hakuwa na matatizo na akagonga mihuri.