Kijana aliyejulikana kwa jina Nchimwa Magidu Ndula (22) mkazi wa Madalawa amefariki dunia baada ya kupigwa fimbo sehemu mbalimbali za mwili wake na baba yake mzazi aitwaye Magidu Ndula Jisusi (55) baada ya kijana huyo kumtorosha binti aliyetaka kumuoa na kumpeleka kwao kama mke .
Kwa mujibu wa Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Singida Stella Mutabihirwa tukio hilo limetokea Oktoba 8, 2021 majira ya saa 10 alfajiri katika kitongoji cha Madalawa kijiji cha Mlandala kata ya Urughu wilaya ya Iramba mkoani Singida.

 Chanzo cha mauaji hayo kinadaiwa kuwa Magidu kwenda katika sherehe za jamii ya kisukuma na kujichagulia msichana kwa utamaduni wa kabila hilo wa 'chagulaga', lakini mzazi huyo hakufurahia hatua hiyo kutokana na kudaiwa mahari kubwa ya ng’ombe.

Kutokana na kutofurahishwa na kitendo hicho, mzazi huyo anadaiwa alipomtaka mwanawe amruhusu msichana kurejea kwao, aligoma.

"Nchimwa Magidu Ndula (22) mkazi wa Madalawa alifariki dunia baada ya kupigwa fimbo sehemu mbalimbali za mwili wake na baba yake mzazi aitwaye Magidu Ndula Jisusi (55) mkazi wa Madalawa

"Jeshi la polisi limefanya uchunguzi wa awali na kubaini kuwa marehemu alipigwa akiwa nje ya nyumba yao alipokuwa anaishi na wazazi wake huku chanzo cha tukio hilo kikibainika kuwa ni mgogoro wa kifamilia uliopelekea kutoelewana baina ya marehemu na mtuhumiwa baada ya marehemu kumtorosha binti aliyetaka kumuoa kutoka kwenye himaya ya wazazi wake na kumpeleka kwao kama mke " ,amefafanua.

Amesema tayari Jeshi la polisi la Polisi mkoa wa Singida linamshikilia Magidu Ndula Jisusi (55) kwa mahojiano zaidi kabla ya kufikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazomkabili.