Kesi ya uhujumu uchumi namba 27 inayomkabili aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro, Lengai Ole Sabaya na wenzake sita, imepigwa kalenda hadi Oktoba 18, mwaka huu, itakaposikilizwa mfululizo kwa wiki nzima.

Ole Sabaya na wenzake, wanakabiliwa na mashtaka matano katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Arusha, likiwamo la matumizi mabaya ya madaraka, utakatishaji wa fedha, kujihusisha na vitendo vya rushwa, kuongoza genge la uhalifu na kujihusisha na vitendo vya rushwa.

Mbali na Ole Sabaya, washtakiwa wengine katika shauri hilo ni Silvester Nyengu (26), Enock Togolani (41), Watson Mwahomange (27), John Odemba, Jackson Macha (29) na Nathan Msuya (31).

Akizungumza mahakamani huko jana, Hakimu wa Mahakama hiyo, Patricia Kisinga, alisema ameahirisha shauri hilo hadi Oktoba 18, mwaka huu na litasikilizwa mfululizo kwa wiki nzima.

Wakili wa Jamhuri, Neema Mbwambo, alidai shauri hilo lilikwenda kwa ajili ya kutajwa na aliiomba mahakama kupanga tarehe ya kusikilizwa kwa kesi.